Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » Dawasa yachangia Kuongezeka kwa Maji; yajipanga kujenga Mitambo ya Majitaka

Dawasa yachangia Kuongezeka kwa Maji; yajipanga kujenga Mitambo ya Majitaka

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Mkuuwa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Paul Makonda akiongea na baadhi ya Viongozi na Watendaji wa Mashirika ya DAWASA na DAWASCO pamoja na Waandishisho wa habari kuhusu Maadhimi ya Wiki ya Maji Duniani yanayoanza leo tarehe 16 hadi kilele chake 22 Machi, 2017 katika Ukumbi wa Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam.


Katibu Tawala Msaidizi wa Huduma za Maji Mkoa wa Dar es Salaam, Bi. Elizabeth Kingu akiongea na baadhi ya Viongozi na Watendaji wa Mashirika ya DAWASA na DAWASCO pamoja na Waandishi wa habari kuhusu Maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani yanayoanza leo tarehe 16 hadi kilele chake 22 Machi, 2017 katika Ukumbi wa Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Maji Safi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASCO) Bw. Kiula Kingu akijibu baadhi ya maswali toka kwa Waandishi wa habari kuhusu Maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani yanayoanza leo tarehe 16 hadi kilele chake 22 Machi, 2017 katika Ukumbi wa Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Meneja Mahusiano ya Jamii Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) Bi. Neli Msuya akifafanua baadhi ya hoja na kujibu maswali toka kwa Waandishi wa habari kuhusu Maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani yanayoanza leo tarehe 16 hadi kilele chake 22 Machi, 2017 katika Ukumbi wa Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya Waandishi wa Habari pamoja na Watendaji toka Mashirika ya DAWASA na DAWASCO wakifuatilia taarifa mbalimbali toka kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Paul Makonda pamoja na Watendaji wa DAWASA na DAWASACO kuhusu Maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani yanayoanza leo tarehe 16 hadi kilele chake tarehe 22 Machi, 2017 katika Ukumbi wa Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam.
 (Picha/Habari na Benedict Liwenga-WHUSM)



Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) imechangia kwa kiasi kikubwa katika kuhakikisha kuwa upatikanaji wa maji safi na salama nchini unaongezeka.



Akiongea leo na Baadhi ya Viongozi na Watendaji wa Mashirika ya DAWASA na DAWASCO pamoja Waandishi wa Habari Jijini Dar es Salaam katika kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani ambayo huadhimisha kila mwaka kuanzia siku ya tarehe 16 hadi 22 Machi, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Paul Makonda amesema kwamba, katika kuadhimisha Wiki hiyo ya Maji, Mkoa wa Dar es Salaam umelenga kuwahamasisha na kuwaelimisha Wananchi, Viongozi wa Serikali za Mitaa pamoja na Kamati za Maji kuhusu namna bora ya usimamizi wa shughuli za maji katika maeneo yao ikiwemo na tarataibu za umiliki wa visima.



Amesema kwamba, lengo la maadhimisho hayo ni kuongeza upatikanaji wa maji, uzalishaji na usambazaji wa maji safi na salama ambayo yatatumika kwa uangalifu ili kupunguza kiwango cha matumizi yake.



Ameongeza kuwa, hali ilivyo sasa, kiwango kikubwa cha Majitaka kutoka viwandani na majumbani kinaachwa kutiririka bila kutibiwa na kurudishwa kutumika tena ambapo jambo hilo husababisha virutubisho vingi vilivyomo katika maji hayo kupotea.



“Katika kuhakikisha maendeleo endelevu na mzunguko wa uchumi, Majitaka ni rasilimali muhimu na hivyo kuyasindika, kuyasafisha kwa kuyatibu na kuyatumia tena ni jambo la lazima”, Alisema Makonda.



Aidha, ameongeza kuwa, katika maadhimisho ya Wiki ya Maji, shughuli za usafi na upandaji miti katika maeneo ya vyanzo vya maji zitafanyika, miradi mitatu ya maji katika maeneo ya Mbagala pamoja na Pugu itazinduliwa na pia miradi 20 ya Jamii itakabidhiwa rasmi DAWASCO.



Amefafanua kuwa, huduma ya maji kwa wakazi wa Dar es Salaam hutolewa na DAWASA ambayo imekodisha shughuli za uendeshaji huduma kwa Shirika la Maji Safi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASCO) ambapo vyanzo vikuu vya maji ni Mto Ruvu, Mto Kizinga pamoja na maji chini ya ardhi.



Mhe. Makondaa ameongeza kuwa, hali ya upatikanaji wa huduma ya maji kwa Wakazi wa Dar es Salaam ni asilimia 75 ambapo uzalishaji wa maji hayo kwa sasa ni lita Milioni 390 kwa siku wakati mahitaji ya maji hayo kwa sasa ni ni lita Milioni 510 kwa siku.


Kuhusu Huduma ya Majitaka, Mhe. Makonda amesema kwamba, mfumo uliopo sasa unahudumia asilimia 10 tu ya wakazi wote wa Jiji, lakini kuna mitambo mitatu ambayo inatarajiwa kujengwa katika maeneo ya Jangwani, Kurasini pamoja na Kunduchi na mifumo mingine 50 midogo itajengwa katika maeneo ambayo yanakumbwa na kipindupindu mara kwa mara.


Makonda ameeleza pia kuhusu miradi ya visima vya dharura katika maeneo yasiyo na maji ya bomba ambapo amesema kwamba, DAWASA ina idadi ya visima 147, Manispaa 789 na Taasisi na Watu binafsi visima 600.


Kuhusu mafanikio katika sekta hiyo, amesema kwamba, moja ya mafanikio yaliyopatikana katika utoaji wa huduma ya maji safi na usafi wa mazingira kwa Mkoa wa Dar es Salaam toka mwaka jana hadi mwezi Machi mwaka huu ni pamoja na kukamilika kwa Mradi Mkubwa wa Ruvu Chini ambao umeongeza upatikanaji wa maji toka lita Milioni 182 kwa siku hadi kufikia lita Milioni 270 kwa siku, pia Mradi Mkubwa wa Ruvu Juu ambao utaongeza upatikanaji wa maji kutoka lita Milioni 82 kwa siku hadi kufikia lta Milioni 196 kwa siku ambapo mradi huu unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Machi mwaka huu baada ya kukamilika kwa kazi ya kuunganisha umeme mkubwa kutoka Chalinze.


“Elimu juu ya maji zitolewazo na Serikali kupitia DAWASA na DAWASCO itatolewa, hivyo DAWASCO wameandaa Madawati maalum kwa wananchi wote katika maeneo yote ya huduma na yatakuwa wazi wiki nzima kuanzia leo tarehe 16 hadi 22 Machi, 2017 kuanzia saa 2:00 asubuhi hadi saa 12:00 jioni kila siku”, alisema Makonda.


Kwa upande wake Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Maji Safi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASCO) Bw. Kiula Kingu amesema kwamba, DAWASCO pamoja na DAWASA wamefanikiwa kuzuia upotevu wa maji kwa kiasi kikubwa ambapo kwa mwaka jana ulikuwa  ni asilimia 47 na mwaka huu umepungua na kufikia asilimia 38.6.


Ameongeza kuwa, wao kama taasisi wamekuwa wakijitahidi kuhakikisha kuwa wanaendelea kupunguza upotevu wa maji kwa kubadilisha miundombinu chakavu ya maji na kuweka miundombinu mipya, pia ubadilishaji wa mita zilizozidi umri wa miaka mitano umeendelea kufanyika hali ambayo imesaidia watu wengi kupata maji.


Naye Meneja Mahusiano ya Jamii Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) Bi. Neli Msuya ameeleza kwamba, maeneo yote ya Dar es Salaam yasiyo na mtandao wa maji yamekuwa yakitengenezewa ramani (design) ili yawekewe mitandao hiyo ya maji ili maji yaweze kupatikana kwa wakazi wa maeneo hayo.


Wiki ya Maji huadhimishwa Duniani kote kuanzia tarehe 16-22 ya mwezi Machi ambapo Kaulimbiu ya Maadhimisho hayo kwa mwaka huu ni “Majisafi na Majitaka-Punguza Uchafuzi yatumike kwa Ufanisi (Water and Waste Water-Reduce and Reuse).

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa