Na. Georgina Misama
MAELEZO
Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli amepongezwa kwa moyo wake wa
kujitoa na kuwajali wanyonge hasa wagonjwa wasiojiweza na wenye uhitaji wa gharama za matibabu.
Hayo yamesemwa leo na
Bi. Neema Mwita Wambura maarufu kama ‘Mgonjwa wa Magufuli’ wakati
alipotembelewa na waandishi wa habari katika Hospitali ya Taifa Muhimbili
ambako alilazwa kwaajili ya kupatiwa matibabu baada ya kupata majeraha ya moto.
“Ninamshukuru sana
Mhe. Rais Magufuli kwa msaada wake katika matibabu yangu. Hivi sasa mimi nina
maendeleo makubwa, naweza kuongea, kula na hata kugeuza shingo yangu.
Nitamuombea Rais Magufuli mpaka siku naingia kaburini, Mungu ambariki” anasema
Neema.
Akisimulia mkasa
uliompata Neema anasema kwamba alimwagiwa maji ya moto na mumewe baada ya
kuchuma mahindi mawili (2) shambani bila ya ruhusa yake. Mumewe huyo alitoweka
na ndugu za Neema walihofia kumchukua kwa kuogopa kudaiwa mahali iliyolipwa na
mumewe kama taratibu za kumuoa.
“Hakuna ndugu yangu
hata mmoja aliyejitokeza kunisaidia kipindi chote cha matibabu. Walihofia kama
ningefariki ingempasa huyo ndugu kurudisha mahali ambayo mume wangu alitoa.
Nilikuwa nasaidiwa na majirani tu, nilikata tamaa ya kuishi nilikuwa nasubiri
siku yangu ya kufariki ifike,” anasimulia Neema.
Aidha, Neema
anawashukuru watumishi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili wodi ya Mwaisela
wakiwemo manesi na madaktari kwa upendo na msaada mkubwa waliompatia toka siku
wanampokea katika hospitali hiyo mpaka sasa ambapo anatarajia kurudi nyumbani.
“Nawashauri
watanzania wasisikilize maneno ya watu wanaolalamika kwamba Muhimbili huduma
sio nzuri, si kweli,kwa muda wote niliokaa hapa nimepatiwa huduma nzuri, tena
kwa upendo na upole”
Akielezea maendeleo
ya afya ya Neema, Mkurugenzi wa Upasuaji ambaye pia ni Daktari bingwa wa
upasuaji Dkt. Ibrahimu Mkoma amesema kwamba, Neema alipokelewa hospitalini hapo
tarehe 06/07/2015 akitokea Mkoa wa Mara wilaya ya Musoma , Neema alikuwa na
majeraha ya mwaka mmoja toka aunguzwe.
Mpaka sasa Neema
ameshafanyiwa oparesheni tatu kwa nyakati tofauti, zilizohusisha kutengenisha
baadhi ya viungo kwani shingo, kifua na mkono wa kushoto vilishikana.
Halkadhalika ilibidi kutoa ngozi ya sehemu ya mwili ili kufunika sehemu zile
zilizoathirika zaidi.
“Ni katika kipindi
hicho cha matibabu, Mhe. Rais alimuona Neema na kuguswa na hali yake, ambapo
aliamua kumsaidia mpaka hivi sasa mnavyomuona. Neema sasa amepona na ataweza
kuihudumia familia yake vizuri”,
aliongeza Dkt. Mkoma.
Akiongelea Moyo wa
kujali wanyonge alionao Rais JPM, Dkt. Mkoma anasema kwamba Rais anaongoza kwa
mfano, hivyo watanzania hawana budi kujifunza moyo huo wa kujali na kusaidia
wahitaji wakati wote kwenye jamii.
Aidha, Dkt. Mkama
ametoa wito kwa wadau na taasisi zinazohusika katika kutoa elimu kwa umma hususan
madhara ya vitendo vya kikatili kutoa elimu hiyo kwa kuzingatia sehemu zenye
ukubwa wa tatizo hilo ili kumaliza kabisa majanga ya aina hiyo.
0 comments:
Post a Comment