Na Mwandishi Wetu.
Hali ngumu ya maisha ikiwepo
ukosefu wa mahitaji muhimu imetajwa kama sababu kubwa inayochochea Biashara
Haramu ya Usafirishaji wa Binadamu huku waaathirika wa biashara hiyo wakiahidiwa
maisha mazuri katika nchi wanazopelekwa.
Akizungumza wakati wa
Ufunguzi wa Mafunzo ya Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Usafirishaji
wa Binadamu, Mwenyekiti wa Sekretarieti ya Kupambana na Kuzuia Biashara Haramu
ya Usafirishaji wa Binadamu (ATP), ambaye pia ni mgeni rasmi
katika mafunzo hayo, Adatus Magere amesema
wahusika wa biashara hiyo wamekua wakiwarubuni waathirika wa biashara
hiyo kuwapatia maisha mazuri na kujikuta
wakiingia katika madhara ya biashara hiyo.
Aliongeza kuwa kuna umuhimu
kwa watunga sheria na vyombo vya sheria kutunga sheria zitakazo saidia
kutokomeza kabisa biashara hiyo kwani imekua ikiendelea kukua siku hadi siku
hali inayopelekea idadi ya wahanga wa biashara hiyo kuendelea kuongezeka.
“Tunaomba watunga sheria na
wasimamiaji wa sheria kusaidiana kwa pamoja katika kudhibiti na kuzuia biashara
hiyo kwa kutoa adhabu kali kwa wale watakaobainika kuhusika moja kwa moja na
biashara hiyo ili tatizo hili liweze kuisha katika nchi zetu,” alisema Magere.
Aidha Katibu Mkuu wa
Sekritarieti ya Kupambana na Kuzuia Biashara Haramu ya Usafirishaji Binadamu ambaye
pia ni mwenyeji kwenye mafunzo hayo, Seperatusi Fella, amesema kuwa ili kuweza
kupambana na kuzuia biashara hiyo kuna umuhimu kwa wadau mbaimbali kutoa elimu
na mafunzo juu ya athari zitokanazo na usafirishaji haramu wa binadamu, hivyo
mafunzo ya mara kwa mara ni muhimu kwa wananchi na wadau mbalimbali.
Naye Mratibu wa mradi wa
Shirika la Wahamiaji la Kimataifa (IOM), Tamara Keating ameahidi kushirikiana na mashirika mbalimbali
ili kukomesha biashara hiyo sambamba na kutoa elimu kwa wananchi ili kupata taarifa ya wahusika wa biashara hiyo.
Ripoti na tafiti mbalimbali
za kimataifa juu ya biashara hiyo zinaonesha Tanzania ni mojawapo kati ya nchi
nyingi zinazohuishwa na biashara haramu ya usafirishaji binaadamu ambapo
waathirika wengi wa biashara hii ni watoto walio chini ya umri wa miaka 18 na kuendelea wanaoahidiwa kazi nzuri
na maisha mazuri pindi wafikapo katika nchi wanazopelekwa.
Mafunzo hayo yanafanyika katika hoteli ya Colosseum jijini Dar es Salaam
yakiwa na lengo la kuleta uelewa wa jinsi biashara hiyo inavyoendeshwa pamoja na
kuleta ushirikiano katika kukomesha biashara haramu ya usafirishaji binadamu
baina ya wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika.
0 comments:
Post a Comment