WATU 479 wameuawa nchini kutokana na vitendo vya ukatili ukiwamo wa
watu kujichukulia sheria mkononi katika kipindi cha nusu mwaka 2017,
ikiwa ni mara tatu ikilinganishwa na mwaka uliopita, jambo linaloonesha
kuwapo ukiukwaji wa haki.
Aidha katika matukio hayo, Mkoa wa Dar es Salaam unaongoza kwa watu
kujichukulia sheria mkononi kwa kuwa na matukio 117 yaliripotiwa polisi,
ukifuatiwa na Mkoa wa Mbeya wenye matukio 33, Mara (28) na Geita (26).
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk
Helen Kijo Bisimba alibainisha hayo jana jijini Dar es Salaam katika
uzinduzi wa ripoti ya hali ya haki za binadamu kwa kipindi cha nusu ya
Mwaka 2017.
Ripoti hiyo inaonesha hali za binadamu kuwa bado ni mbaya kwa kipindi
cha nusu mwaka ikilinganishwa na miaka iliyopita. Dk Bisimba alisema
ripoti hiyo inayoanzia Januari hadi Juni mwaka huu inaonesha kuwepo kwa
ukiukwaji mkubwa wa haki za kiraia hususani haki ya kuishi, lakini pia
ukiukwaji mkubwa wa haki za makundi maalumu wakiwemo wanawake na watoto.
Kuhusu kujichukulia sheria mkononi, alisema taarifa za Jeshi la
Polisi zinaonesha kuwa matukio ya mauaji kwa watu kujichukulia sheria
mkononi yamekuwa yakipungua kwa kati mwaka 2013 mpaka 2016 kutoka vifo
597 mpaka vifo 135. “Hata hivyo, matukio hayo imeonekana kujirudia tena
kwa kasi ambapo na kufikia mara tatu ya idadi ya mwaka jana,” alisema
Bisimba.
Alisema Jeshi la Polisi linapaswa kushughulikia haraka tatizo la
kuwapo matukio hayo na kuhakikisha watuhumiwa wa matukio hayo
wanafikishwa mbele ya sheria. Aidha, Bisimba alisema Wizara ya Mambo ya
Ndani na Jeshi la Polisi kwa pamoja yanatakiwa kuhakikisha kuwa askari
wanaotuhumiwa kufanya mauaji ya raia wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa
sheria.
Kuhusu haki za wanawake na watoto alisema matukio ya ukiukwaji wa
haki za makundi hayo yameendelea kuripotiwa kwa kiwango kikubwa nchini
na taarifa ya Jeshila Polisi kwa kipindi cha Januari hadi Machi,
inaonesha kumekuwa na matukio 2,059 ya ubakaji yaliyoripotiwa katika
vituo mbalimbali. Mtafiti wa LHRC, Fundikila Wazambi alisema ripoti hiyo
inatokana nautafiti mbalimbali uliofanywa na kituo hicho wenye lengo la
kuangalia ukiukwaji wa haki za binadamu.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment