WANANCHI waliokuwa wakiishi kinyume na utaratibu kwenye Bonde la
Jangwani jana walijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kupambana na jeshi
la polisi kuzuia bomoabomoa ambayo ilikuwa ikiendeshwa na Jiji katika
eneo hilo.
Katika mapambano hayo ambayo jeshi la Polisi liliweza kutuliza hali
ya vurugu, gari la mwendo kasi pamoja na daladala zilivunjwa vioo
kutokana na mawe waliyokuwa wakirusha, lakini pia askari watano wakiwamo
wawili wa jiji na watatu wa Jeshi la Polisi walijeruhiwa. Hadi Polisi
wanadhibiti vurugu hizo, wakazi hao walisababisha usumbufu kwa watumiaji
wa barabara hiyo kwa zaidi ya saa tatu kuanzia saa tatu asubuhi.
Kwa mujibu wa mwandishi wetu aliyekuwa kwenye eneo la tukio, alisema
kuwa bomoabomoa ilianza saa 3:00 asubuhi lakini wananchi hawakukubali na
kuanza kuwarushia mawe na chupa askari wa Jiji ambao walikuwa
wanasimamia kazi hiyo. Ilipofika saa 5:00 asubuhi, askari wa jeshi la
polisi kwa ajili ya kutuliza ghasia waliwasili ndani ya saa moja na
kuweza kudhibiti vurugu hizo kwa kuwatawanya watu hao. Katika mapambano
hayo, jeshi la polisi lilifanikiwa kuwakamata baadhi ya watu na
kuwapakiza katika gari maalumu lililokuwa limewekwa katika eneo hilo.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment