Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » DAR WAFURIKA KUAGA WALIOKUFA UGANDA

DAR WAFURIKA KUAGA WALIOKUFA UGANDA



Imeandikwa na Evance Ng'ingo


Naibu Waziri wa zamani, Gregory Teu akitoa heshima za mwisho kwa miili ya watu 13 wa familia yake kwenye ibada ya kuaga miili hiyo iliyofanyika katika Hospitali Kuu ya Jeshi Lugalo, Dar es Salaam jana.
WINGI wa watu uliojitokeza katika Hospitali Kuu ya Jeshi ya Lugalo jijini Dar es Salaam jana, kuaga miili 13 ya Watanzania waliokufa kwenye ajali ya gari nchini Uganda mapema wiki hii, ulisababisha eneo lililotengwa la kuaga miili hiyo, kujaa na hadi wengine walilazimika kuzuiliwa kuingia eneo hilo.
Watanzania hao wapoteza maisha kutokana na ajali ya iliyohusisha basi dogo la kukodi aina ya Toyota Coaster lenye namba za usajili T540 DLC wakati wakitokea Kampala nchini Uganda, kuhudhuria harusi baina ya daktari binti wa Kitanzania, Dk Annette Gregory Teu na mumewe, Dk Treausuer Ibingira ambaye ni raia wa Uganda.
Bi harusi ambaye ni binti wa aliyekuwa Naibu Waziri katika Serikali ya Awamu ya Nne, Dk Gregory Teu, pamoja na mumewe Dk Ibingira walikuwapo jana msibani pamoja na ndugu wengine wa bwana harusi kutokea Uganda, ambayo iliwakilishwa na Waziri anayeshughulikia Jiji la Kampala, Betty Namisango.
Akizungumza kwa niaba serikali, Waziri wa Nchi, Ofisi wa Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora), Angella Kairuki alitoa salamu za rambirambi kwa niaba wa serikali na Watanzania kwa ujumla, na kuzipa pole familia za wafiwa.
Kairuki alisema, “serikali imesikitishwa sana na ajali hii ambayo imechukua maisha ya wenzetu 13 na tena kwa pamoja, tunawapa pole wote ambao wamekutwa na msiba huu na tunawatakia safari njema mnapoenda kuwapumzisha kwenye nyumba yao ya milele.”
Katika shughuli hiyo, pia walikuwapo Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi, na mawaziri Charles Mwijage (Viwanda, Biashara na Uwekezaji) na Profesa Palamagamba Kabudi (Katiba na Sheria).
Wakati wa kuaga miili hiyo, vilio vilitawala huku karibu kila mmoja akitaka kumuaga mpendwa wake, kutokana na wingi huo wa watu waliokuwa wakitaka kuiaga miili hiyo, ilisababisha kuzuiliwa kwa watu wengine na badala yake ndugu wa karibu tu na viongozi walipata wasaa wa kuaga.
Miili hiyo imesafirishwa kwenda katika mikoa mitatu ya Kilimanjaro, Arusha na Dodoma wilayani Mpwapwa, ambako leo watazikwa. Dk Teu ni mwenyeji wa Mpwapwa ambako alihudumu kwa miaka mitano kama mbunge kuanzia mwaka 2010 hadi 2015.
Miili hiyo iliwasili nchini juzi usiku kwa ndege na baada ya kuwasili, ilipokelewa na wanajeshi wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na kupelekwa moja kwa moja hadi Hospitali Kuu ya Jeshi ya Lugalo, kupumzishwa kabla ya kuagwa jana asbuhi.
Waliopoteza maisha ni mtoto wa kwanza wa Naibu Waziri huyo wa zamani aitwaye Sakazi, baba yake mzazi George Teu, baba mdogo wake, Mazengo Teu, dada yake Rehema Teu, wadogo zake Esther Teu na Alfred Teu na shangazi Paulina Ndagala.
Pia yupo shemeji wa Naibu Waziri huyo, Happy Soka, Bonny Njenga, kaka wa Teu, Edwin Kimario, baba mdogo wake Vivian Mchaki, rafiki wa bi harusi huyo, Aneth, Dk Eibnoth Laizer ambaye alikuwa ni mmoja wa wapambe wa bibi harusi kwenye sherehe hiyo.
Majeruhi wanaoendelea na matibabu nchini Uganda ni mdogo wa Teu, Erasto Teu, rafiki mwingine wa bi harusi, Dk Irene Lyatuu, mke wa marehemu Njenga aitwaye Dativa Shayo na ndugu wa karibu.
CHANZO HABARI LEO 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa