Home » » WALIOKUTWA NA MADINI YA MILIONI 500, WAHUKUMIWA KULIPA FAINI YA MILIONI 3 AU JELA MIAKA MIWILI

WALIOKUTWA NA MADINI YA MILIONI 500, WAHUKUMIWA KULIPA FAINI YA MILIONI 3 AU JELA MIAKA MIWILI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Wafanyabiashara wa madini, wakitoka mahakamani baada ya kupatikana na hatia na kuhukumiwa kulipa faini ya sh. Milioni Tatu au kwenda jela miaka miwil
Na Karama Kenyunko, blogu ya jamii.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewahukumu watanzania  watatu wanaofanya biashara ya madini kulipa faini ya sh. Milioni tatu ama kwenda jela miaka miwili baada ya kupatikana na hatia kwa makosa ya kusafirisha dhahabu ya zaidi ya milioni 507. Aidha mahakama imetaifisha madini hayo ya dhahabu yenye uzito wa kilo 6.242 yenye thamani ya Sh 507,347,241.11 kuwa mali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Hatua hiyo imekuja baada ya washtakiwa hao Mashaka Lucas, Jafarri Hussein na mwenzao, Akifu Mohamed waliokuwa wakikabiliwa na mashtaka mawili ya kukutwa na kusafirisha madini hayo bila ya kuwa na vibali kukubali makosa hayo na kutiwa hatiani.

Hukumu hiyo imesomwa na Hakimu Mkazi Mkuu,Huruma Shaidi.  Akisoma hukumu hiyo  Hakimu Shaidi amesema, mahakama imezingatia taarifa kutoka upande wa mashtaka kuwa washtakiwa ni wakosaji kwa mara ya kwanza na wamekubali makosa ingawa mshtakiwa Mashaka na Jafarri wanaleseni za kuendesha biashara hizo lakini suala ni kukutwa na madini hayo na kuyasafirisha bila ya kuwa na vibali.

 “Lengo la mahakama siyo kumfanya mtu aondoke katika kile alichokifanya bali ajutie" Amesema Hakimu Shaidi.

Kufuatia hayo, mahakama imemuamuru kila mshtakiwa kulipa faini ya Sh milioni 1.5 katika kila kosa hivyo kila mshtakiwa atapaswa kulipa Sh milioni 3 na iwapo watashindwa watatumikia kifungo cha miaka miwili gerezani. Kuhusu gari aina ya Noah walilokamatwa nalo washtakiwa hao siku ya tukio  Bandarini eneo la Azam, Hakimu Shaidi alisema mahakama inashindwa kutoka amri kwa sababu upande wa  mashtaka haukupeleka kadi ya gari hilo wala gari lenyewe mahakamani hapo kama kielelezo.

Kabla ya hukumu kusomwa, Wakili wa Serikali Jehovaness Zacharias aliiambia mahakama kuwa hawana kumbukumbu za makosa ya nyuma za washtakiwa Ila aliomba wapewe adhabu Kali ili iwe fundisho kwa wengine.

Pia aliomba mahakama itoe oda ya kutaifishwa kwa madini pamoja na gari aina ya Noah walilokamatwa nalo washtakiwa hao Bandarini eneo la Azam. Hatua hivyo Mawakili wa washtakiwa hao,Hadson Ndusyepo na Evodius Mtawala waliiomba mahakama iwatazame kwa jicho la huruma washtakiwa hao.

Alidai kuwa washtakiwa hao wanajihusisha na shughuli za madini katika maisha yao , kujipatia kipato na wana leseni halali. Kwa kutokuelewa utaratibu wa madini ndio wamejikuta katika tatizo hilo, ndio maana hawakupenda kuisumbua mahakama wakakubali ili waweze kuendelea na shughuli zao za ujenzi wa Taifa.

Katika kesi ya msingi,washtakiwa Jafarri na Akifu  wanakabiliwa na shtaka la kukutwa na vipande vitano vya madini ya dhahabu vyenye uzito wa kilo 6.242 vyenye thamani ya Sh 507,347,241.11bila ya kuwa na kibali.

Pia washtakiwa Mashaka, Jafarri na Akifu wakiwa Bandarini eneo la Azam wanadaiwa kuyasafirisha madini hayo bila ya kuwa na vibali.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa