Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » FIRE KLABU ZITUMIKE KUZUIA MAJANGA YA MOTO SHULENI.

FIRE KLABU ZITUMIKE KUZUIA MAJANGA YA MOTO SHULENI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Emmanuel Kibona akitoa elimu ya Kinga na Tahadhari Dhidi ya Majanga ya moto kwa Walimu na Wanafunzi wa Shule ya Secondari Azania (Picha na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji)


Picha ni sehemu ya bweni iliyoathirika na moto na kuteketeza mali za Wanafunzi. (Picha na Maktaba)



Na Nasibu Mgosso.
Jeshi la  Zimamoto na Uokoaji ndicho chombo chenye jukumu la kuzuia na kukabiliana na majanga  mbalimbali   kama mafuriko , Tetemeko la  Ardhi,  ajali  za vyombo vya usafiri na usafirishaji,  kuporomoka kwa majengo, migodi,  pamoja na matukio ya moto. 
Mara kwa mara, majanga ya moto yamekuwa yakitokea katika jamii yetu kwa sababu moto ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku.  Utafiti umethibitisha  kwamba,  vyanzo vingi vya moto ni sisi wenyewe (binadamu)  kutokana na uzembe,   hujuma  au kutokukuwa na  elimu ya Tahadhali na Kinga  Dhidi ya  Moto.
Aidha, matukio ya moto yamekuwa  yakitokea mara kwa mara katika shule za bweni hapa nchini  hususani shule za sekondari,  na kusababisha  uharibifu wa miundo mbinu kama vile Mali, majengo na wakati mwingine majeraha au vifo kwa wanafunzi wetu na kuleta simanzi na sintofahamu kwa Wananchi na Taifa kwa ujumla .
Uchunguzi  wa moto (Fire Investigation)  umebaini     sababu  za matukio hayo ni matumizi mabaya ya umeme yanayofanywa na   wanafunzi  kwa  kujiunganishia nyaya za umeme wenyewe bila kuwa na weledi iliwapate  sehemu za kuchaji simu na heater za kuchemshia maji kwa kificho kwa sababu Wanafunzi  hawaruhusiwi kuwa na simu wala heater pindi wanapokuwa shuleni.
Lakini pia sababu nyingine ni matumizi ya mishumaa, unapokatika umeme wakati wa kujisomea. Shule nyingi  zinajaribu kuzuia mabweni kutumika kama sehemu za kujisomea,  lakini  bado wapo baadhi ya Wanafunzi  wanaamua   kujisomea  ndani ya  mabweni  bila kuchukua  tahadhari yoyote na wanapopitiwa na usingizi,  uacha mishumaa inaendelea kuwaka na hatimaye kusababisha ajali ya moto.
Utakumbuka miaka kadhaa iliyopita matukio kama haya ya kuungua kwa shule yalileta majonzi  makubwa kwa kuangamiza  maisha ya Wanafunzi wengi.  Kuungua kwa shule ya Shauritanga Mkoani Kilimanjaro mwaka 1994 ambapo zaidi ya wanafunzi 40 walipoteza Maisha pamoja na Mali.
Mwaka 2009 shule ya sekondari Idodi Mkoani Iringa iliteketea kwa moto na zaidi ya wanafunzi 20 walipoteza Maisha pamoja na Mali. Hiyo ni mifano tu lakini matukio ya kuungua kwa shule ni mengi sana hapa nchini.
Ili kupunguza matukio hayo, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limeanzisha Fire klabu  katika shule mbalimbali  za Msingi na Sekondari ili kupata wajumbe  watakaoliwakilisha  katika shule na makazi yao.
Kwa kutumia fire klabu, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji  limejenga ukaribu mkubwa na Wanafunzi wa shule hizo,  hatua inayosaidia kuwapa elimu stahiki ya kukabiliana na majanga ya moto.
Changamoto  iliyopo ni  mapokeo ya baadhi ya Viongozi wa shule kutokuwa tayari kuruhusu shule zao kuanzisha  klabu za Zimamoto zinazosimamiwa na  kuratibiwa na Jeshi hilo ambapo mpaka sasa ni shule 100 ndizo zilizofungua klabu hizo kwa nchi nzima.
Kama nilivyo eleza hapo mwanzo, lengo la klabu hizo ni kuwapa fursa wanafunzi kuwa familia moja na wataalamu wa Zimamoto. Ukaribu huo hutumika kwa wazimamoto kuwapa mbinu mbalimbali za kuzuia na kukabiliana na vyanzo vya moto.
Lakini  kwa upande wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji,  ni kupanua wigo wa kuwa na idadi kubwa ya  watu, wanaoifahamu vyema  elimu  hiyo  na kuwa  mabalozi  wazuri  watakao liunganisha Jeshi  na jamii kwa kufikisha  elimu hiyo, Mijini  na Vijijini na hatimaye kuweza kupunguza na kutokomeza kabisa majanga.
Wito wangu kwa wamiliki wa shule, walipokee jambo hili kama ukombozi kwao kupunguza majanga  ya moto katika shule zao.
Tukishirikiana tutapunguza majanga ya moto, na Taifa litakuwa salama.
Mungu ibariki Afrika Mungu ibariki Tanzania.



0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa