Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » RAIS KIKWETE AONGOZA KUUAGA MWILI WA MWAKAPUGI DAR

RAIS KIKWETE AONGOZA KUUAGA MWILI WA MWAKAPUGI DAR

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Rais Jakaya Kikwete jana aliongoza mamia ya waombolezaji kuaga mwili wa aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Arthur Mwakapugi tayari kwa ajili ya kusafirishwa leo kwenda kuzikwa kijijini kwake Ilundo, Wilaya ya Tukuyu mkoani Mbeya.
Mwakapugi, ambaye alifariki dunia akiwa na miaka 64, alitumikia taifa kwa miaka 30 mfululizo kabla ya kufikwa na mauti Ijumaa saa 3:45 usiku katika Hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam.
Rais Kikwete ambaye aliwasili msibani majira ya saa 11 jioni, nyumbani kwa marehemu Mikocheni B, alitia saini katika daftari la wageni kabla ya kutoa heshima za mwisho.
Wengine waliotoa heshima zao ni pamoja na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, Katibu Mkuu Kiongozi Ombeni Sefue, Katibu Mkuu wa Nishati na Madini Eliakim Maswi na aliyekuwa Katibu Mkuu, David Jairo pamoja na manaibu makatibu wakuu wengine kutoka wizara mbalimbali.
Msemaji wa familia ambaye pia ni mjomba wa marehemu, Mathias Mwambona alisema pamoja na marehemu kustaafu kazi kwa muda mrefu, serikali kupitia wizara ya nishati na madini imeonyesha moyo wa kujali, kuthamini mchango wake kutokana na mwitikio waliouonyesha.
“Tunaishukuru sana Serikali pamoja na viongozi, jamaa na marafiki kwa ujumla, upendo uliojionyesha hauwezi kupimwa kwa kipimo chochote, wizara na mfanyakazi mmoja mmoja ndiyo wamekuwa mchango mkubwa katika hatua zote za msiba, kama familia tunawashukuru sana,” alisema.
Mwakapugi aliyeacha mjane na watoto wawili, alitumikia nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwamo Shirika la Viwango nchini (NBS), Mkurugenzi wa Tume ya Mipango 1999 mpaka 2006 kabla ya kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini tangu mwaka 2006 mpaka 2010.
Baada ya kustaafu mwaka 2010, Mwakapugu aliendelea kufanya kazi katika taasisi nyingine zinazojihusisha na masuala ya kiuchumi kupitia Taasisi ya Utafiti ya Kuondoa Umaskini (Repoa).
Chanzo:Mwananchi

1 comments:

Anonymous said...

ni wilaya ya rungwe sio tukuyu

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa