Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » AFIKISHWA KORTINI

AFIKISHWA KORTINI

Mwenyekiti Wa Cuf, profesa Ibrahim Lipumba, akiwa kizimbani mahakama ya hakimu mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam jana.
 
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba, amepatwa na shinikizo la damu la ghafla wakati akisubiri hati ya mashitaka akiwa mikononi mwa Jeshi la Polisi ofisi za makao makuu ya Kanda Maalumu ya Jeshi hilo, jijini Dar es Salaam.
 
Kufuatia mshtuko huo, Prof. Lipumba alitolewa kituoni hapo kimya kimya na kuingizwa kwenye gari la polisi lenye namba za usajili TP 2566 na kukimbizwa Hospitali ya UN, iliyopo eneo la Kinondoni, jijini kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
 
Tukio hilo lilitokea jana baada ya Prof. Lipumba na wafuasi wa CUF takribani 40, kuripoti kituoni hapo kwa ajili ya kuitikia wito wa jeshi hilo kuripoti polisi baada ya kuwatia mbaroni juzi jioni walipokuwa wakijiandaa kuandamana kwa amani kutoka ofisi za CUF Wilaya ya Temeke kuelekea eneo la mkutano wa hadhara Zhakem, Mbagala kwa ajili ya kumbukumbu ya miaka 14 ya mauaji ya wenzao zaidi ya 30 waliouawa mwaka 2001 na polisi katika maandamano ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2000.
 
Prof. Lipumba alikutwa na maswahibu hayo jana saa 6:30 mchana wakati akiwa chini ya uangalizi wa polisi kituoni hapo kwa takribani saa tatu akisubiri hati ya mashitaka kwa ajili ya kupelekwa mahakamani.
 
Awali, Prof. Lipumba aliwasili kituoni hapo akiwa kwenye gari lake lenye namba za usajili T467 BLJ, saa 4:42 asubuhi akitanguliwa na wafuasi wa chama chake kwa takribani nusu saa.
 
PROF. LIPUMBA AZUNGUMZA
Baada ya Mwenyekiti huyo na wenzake kuhojiwa na jeshi hilo kwa takribani dakika 30, alizungumza na waandishi wa habari waliokuwa wamefurika eneo hilo akisema kwamba aliitwa kituoni hapo kwa ajili ya kuhojiwa.
 
“Tumehojiwa na tumetakiwa kila mmoja kuwaleta wadhamini wawili watumishi wa serikali, lakini kutokana na masharti hayo, wanasheria wetu walizungumza na Jehi la Polisi ili kuwaomba kwamba itawawia vigumu kuwapata wadhamini hao kutokana na makosa yanayotukabili. Hivyo tumejidhamini sisi wenyewe na kesho (leo) saa mbili asubuhi tutakuwa hapa kwa ajili ya kuchukua hati ya kupelekwa mahakamani,” alifafanua Prof. Lipumba.
 
Akizungumza kuhusu vurugu hizo, mwanasiasa huyo mkongwe alisema wameshtakiwa kwa kosa la kuandamana bila kibali maalum cha kufanya hivyo kutoka kwa jeshi hilo, sababu  ambayo aliipinga.
 
Alisema aliliandikia jeshi hilo barua ya kuomba kibali Januari 22, mwaka huu, lakini hakujibiwa hadi Januari 26 saa 12 jioni, kuwa maandamano yamezuiliwa, wakati tayari ameshaondoka ofisini na wanachama wa chama hicho wameshafanya maandalizi.
 
“Nilichokifanya jana (juzi), siyo maandamano bali nilikuwa nakwenda kuwazuia wanachama ambao tayari walikuwa wameshajiandaa kwa ajili ya maandamano na mikutano ya hadhara,” alisema Prof. Lipumba na kuongeza:
 
“Asubuhi siku ya pili nilikwenda kuwataarifu wanachama wa CUF Temeke kuhusu kuahirishwa kwa  maandamanao hayo. Wakati nakwenda  Mbagala kuwapa taarifa vijana waliokuwa wameshakusanyika katika viwanja vya Zakhem nilikutana na askari ambao walinizuia na kuanza kunihoji. Baada ya kutoa maelezo yangu walinielewa, lakini baada ya muda mfupi nilishangaa kuona hali imebadilika baada ya kupokea simu kutoka kwa mkuu wa polisi aliyeamuru tufukuzwe.”
 
Alisema kufuatia amri hiyo, walianza kufanyiwa vurugu ambazo ziliwasababishia wafuasi wanne wa chama hicho kujeruhiwa akiwamo Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa chama, Sheweji Mketo na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Chama,  Abdul Kambaya.
 
Kufutia kitendo hicho, Prof. Lipumba alilitupia lawama Jeshi la Polisi na kudai kuwa linafanya kazi kwa shinikizo la siasa na kwamba yeye na chama chake wako imara na wataendelea kupambana hadi mwisho.
 
“Siku zote mfa maji haishi kutapatapa. Suala hili linaonyesha wazi kuwa Chama Cha Mapinduzi kimeishiwa hoja ndiyo maana kinatumia nguvu za jeshi kuzima demokrasia za upinzani,” alisema.
 
Aliongeza kuwa huo ni mwanzo wa mapambano na kwamba  wataendelea kufanya mikutano yao kwani kila mwaka wamekuwa wakifanya kumbukumbu ya mauaji ya wenzao bila kizuizi, lakini alishangaa sababu zilizofanya wazuiliwe mwaka huu.
 
Mkurugenzi wa Mawasiliano wa chama hicho, Abdul Kambaya, alisema analishngaa jeshi hilo kutumia zana za kutengenezea magari kama vile koleo kwa ajili ya kuwadhibiti wahalifu.
 
“Nilipigwa na spana ya kufungulia magari hapa kichwani, ninavyoongea hadi sasa bado kichwa changu kinavuja damu. Jeshi la Polisi halitendi haki na haliwezi kutumia zana ngumu kuwaadhibu watuhumiwa. Mimi nimepasuliwa kichwani, wenzangu kwenye mabega na mgongoni, hivi hawana silaha au walikuwa na dhamira ya kutuua?” alihoji Kambaya.
 
Baadhi ya wananchi waliokuwa katika maeneo hayo, walikilaani kitendo kilichofanywa na jeshi hilo kwani wamemdhalilisha Mwenyekiti huyo.
 
AFIKISHWA KORTINI
Wakati huo huo, Prof. Lipumba jana alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akikabiliwa na mashitaka ya kushawishi wanachama kutenda kosa la jinai.
 
Profesa Lipumba alisomewa mashitaka hayo saa 9:22 alasiri mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi, Isaya Arufani.
 
Kabla ya kusomewa mashitaka hayo, saa 7:45, Prof. Lipumba, alifikishwa katika viunga vya mahakama hiyo akiwa chini ya ulinzi wa askari kanzu.
 
Watu wanaodaiwa kuwa wanachama wa chama hicho walifurika katika viunga hivyo huku wakiwa kwenye makundi wakijadili kuhusu kiongozi wao kufikishwa mahakamani.
 
MASHITAKA
Upande wa Jamhuri ukiongozwa na Mawakili wa Serikali, Joseph Maugo na Hellen Moshi, ulidai kuwa kati ya Januari 22 na 27, mwaka huu mshtakiwa akiwa kama Mwenyekiti wa CUF mahali tofauti jijini Dar es Salaam, aliwashawishi wafuasi wa chama hicho kutenda kosa la jinai.
 
 
Maugo alidai kuwa mashitaka yanayomkabili mshtakiwa yana dhamana kwa mujibu wa sheria na kwamba upande wa Jamhuri hauna pingamizi la dhamana dhidi ya mshtakiwa.
 
“Mheshimiwa hakimu, upelelezi wa kesi hii bado haujakamilika tunaomba tarehe nyingine ya kutajwa” alidai Maugo.
 
Hakimu Arufani alisema mshtakiwa anatakiwa kusaini hati ya dhamana yenye thamani ya Sh. milioni 2 na wadhamini wawili watakaosaini hati yenye thamani hiyo ya fedha.
 
Hilda Mria, Diwani wa Kinondoni wa CUF na Mbunge wa Viti Maalum, Kuruthumu Mchuchuri, walimdhamini Mwenyekiti huyo.
 
Hakimu alisema mshtakiwa yuko nje kwa dhamana hadi Februari 26, mwaka huu kesi itakapotajwa.
 
 
CHANZO: NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa