USAJILI wa mbio za Uhuru Marathon ulioanza kwa kishindo wiki
iliyopita pale Spika wa Bunge, Anne Makinda alipowaongoza wabunge
kufanya hivyo, unazidi kushika kasi huku Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni
ya Mwananchi Communications, Tido Mhando, naye akiahidi kujitosa leo
ili aweze kushiriki.
Akizungumza na Tanzania Daima jana, Katibu wa Kamati ya
Uhuru Marathon, Innocent Melleck, alisema Mhando anatarajiwa kujisajili
kushiriki mbio hizo, baada ya kuvutiwa na lengo lake ambalo ni
kuimarisha amani, umoja na mshikamano.
Melleck hakutaka kufafanua Mhando anataka kushiriki mbio za kilomita
ngapi, ingawa alisema fomu zitatolewa kwa sh 100,000 kwa wale
watakaokimbia mbio za kilomita tatu, sh 2,000 kilomita tano, sh 6,000
kwa atakayeshiriki moja kati ya mbio za kilomita 21 na 42.
“Hizi mbio ni muhimu zaidi kwa ajili ya taifa letu, hivyo ni vyema
kwa Watanzania wote wakashiriki ili kuipigania amani iliyopo nchini
mwetu na ndiyo maana hata Rais Jakaya Kikwete, pia atashiriki. “Kesho
(leo), Tido anatarajiwa pia kujisajili kwa ajili ya kushiriki mbio
hizo, lengo kubwa ikiwa pia kushawishi Watanzania wengine waweze
kushiriki,” alisema.
Mratibu huyo aliongeza kuwa mbio za kilomita 3 zitakuwa maalumu kwa
ajili ya viongozi wa kada mbalimbali, wakiwemo pia wale wa dini na zile
za kilomita 5 pia zitakuwa za kuchangia kwa ajili ya watu wa mahitaji
maalumu.
Mbio hizo zinatarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam Desemba 8 na zitaanzia na kuishia viwanja vya Leaders, Kinondoni.
Chanzo;Tanzania Daima
|
0 comments:
Post a Comment