Home » » Kibanda, Makunga hukumu yao leo

Kibanda, Makunga hukumu yao leo

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, leo inatarajia kutoa hukumu ya kesi ya uchochezi inayomkabili Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari, Absalom Kibanda na wenzake wawili.
Hukumu hiyo itatolewa na Hakimu Mkazi, Waliarwande Lema, ambaye anasikiliza kesi hiyo. Katika kesi hiyo washtakiwa wengine ni Meneja Uendelezaji Biashara wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), Theophil Makunga na mwandishi, Samson Mwigamba.
Makunga na wenzake Absalom Kibanda na Samson Mwigamba wanakabiliwa na kesi ya uchochezi dhidi ya askari wa majeshi ya ulinzi kwa kuchapisha makala kwenye Gazeti la Tanzania Daima yenye maneno yaliyolenga kuwashawishi wasitii viongozi wao.
Makala hiyo ya Novemba 30, 2012 ilikuwa na kichwa cha habari kisemacho;"Waraka maalumu kwa askari wote." Makala hiyo iliandika na mshtakiwa wa kwanza, Mwigamba.
Novemba 25, mwaka jana mahakama hiyo ilifunga utetezi katika kesi hiyo baada ya washtakiwa kupitia kwa mawakili wao kuwasilisha kwa maandishi majumuisho ya mwisho ya kuomba mahakama iwaone hawana hatia.
Wakati huo huo, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu itatoa uamuzi wa Pingamizi la Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) dhidi ya maombi ya dhamana ya raia wa China wanaokabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi kesho kutwa.
Katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi inayowakabili raia hao wa China, upelelezi umekamilika ambapo watasomewa maelezo ya awali Februari 4, mwaka huu. Washtakiwa hao ni Huang Gin Xu Fujie, Chen Jinzha na wanakabiliwa na kesi ambapo kesi hiyo ipo mbele ya Hakimu Mfawidhi, Isaya Arufani.
Ilidaiwa na wakili wa Serikali, Tumaini Kweka, kuwa washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka ya kukutwa na pembe za ndovu, shehena ya pinde 706, vyenye uzito wa kilo 1,880 zikiwa na thamani ya sh. bilioni 5.
Kupitia kwa mawakili wao, Wachina hao wamewasilisha maombi ya dhamana Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, wakiomba wapewe dhamana, baada ya Mahakama ya Kisutu kuwanyima dhamana kutokana na kutokuwa na uwezo wa kisheria kusikiliza kesi hiyo.
Katika maombi hayo ya dhamana namba 14 ya mwaka 2013, Wachina hao kupitia kwa mawakili wao, Edward Chuwa na Richard Rweyongeza, wanadai kuwa dhamana ni haki yao kwa mujibu wa Katiba.
Maombi hayo yalitarajiwa kusikilizwa jana na Jaji Rose Teemba, lakini yalikwama, baada ya kila upande katika kesi hiyo kuweka pingamizi dhidi ya upande mwingine.
Awali, DPP aliwasilisha hati ya kupinga dhamana ya washtakiwa hao akiiomba mahakama hiyo isiwape dhamana, akibainisha kuwa ni kwa maslahi ya Taifa.
Hata hivyo mawakili wa washtakiwa nao waliweka pingamizi dhidi ya hati ya DPP kuiomba mahakama iitupilie mbali, wakidai kuwa limewasilishwa mahakamani isivyo halali.
Mawakili hao, Chuwa na Rwe y o n g e z a kwa n y a k a t i tofauti walifafanua kuwa sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai iliyotumika katika hati hiyo haitumiki katika kesi hiyo.
Pia mawakili hao walieleza kuwa hati hiyo imewasilishwa kabla ya wakati, huku wakibainisha kuwa ilipaswa kuwasilishwa baada ya upelelezi kukamilika. Akijibu hoja hizo, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Faraja Nchimbi alisema kuwa Sheria iliyotumika katika hati hiyo ni sahihi kwa kuwa sheria zote yaani CPA na Sheria ya uhujumu uchumi zinaweza kutumika katika shauri hilo.
Pia SSA Nchimbi alisema kuwa DPP anaweza kuwasilisha hati ya kuzuia dhamana ya washtakiwa mahakamani wakati wowote na si lazima mpaka upelelezi uwe umekamilika.
Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Jaji Teemba aliahirisha shauri hilo hadi keshokutwa, Ijumaa kwa ajili ya uamuzi wa uhalali wa hati ya DPP kuwepo mahakamani kuzuia dhamana ya washtakiwa hao, kabla ya kusikiliza maombi ya msingi ya dhamana.
Wachina hao walikamatwa na nyara hizo katika nyumba walimokuwa wakiishi, mapema Novemba mwaka huu.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa