Home » » TASO yataka wanachama kujiandaa Nanenane

TASO yataka wanachama kujiandaa Nanenane

CHAMA cha Wakulima Tanzania (TASO) kimewataka wakulima, wafugaji, wavuvi na wadau mbalimbali kujiandaa kikamilifu ili kushiriki Maonesho ya Nanenane yanayotarajia kufanyika Agosti Mosi, Kanda ya Kusini na kufikia kilele Agosti 8, mwaka huu.
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa Dar es Salaam jana na kusainiwa na Mwenyekiti wa TASO, Engelbert Moyo, ilisema kuwa wadau hao ndiyo walengwa wa maonesho hayo hivyo hawana budi kujiandaa kikamilifu ili kuweza kushiriki vyema.
Alisema sherehe za maonesho hao zinatarajia kufanyika katika Uwanja wa Maonesho ya Kilimo wa Ngongo uliopo Mjini Lindi na kwamba kulingana na taratibu za uendeshaji maonesho hayo yatafanyika kwa miaka mitatu mfululizo katika Kanda ya Kusini.
"Moja ya malengo ya TASO ni kushirikiana na Serikali katika kuendeleza Viwanja vya Maonesho ya Kilimo nchini, kuandaa sherehe na maonesho ya kilimo na Nanenane kitaifa kwa zamu kikanda kila baada ya miaka mitatu, hivyo mwaka huu maonesho ya kilimo yatafanyika kitaifa kwa mara ya kwanza Kanda ya Kusini,"alisema Moyo.
Alisema madhumuni makubwa ya maonesho ya Nanenane ni kutoa msukumo maalumu nchini kote katika kuinua kiwango cha kilimo, ufugaji, uvuvi, ufugaji wa nyuki na kuimarisha ushirika na pia kuhimiza hifadhi ya mazingira na kuwatukuza wahusika hao wote kwa mchango mkubwa wanaoutoa katika kuendeleza nchi.
"Sehemu kubwa ya sherehe hizo huwa ni maonesho ya kilimo ambayo lengo lake kubwa ni kutoa mafunzo, elimu bora ya kilimo na ufugaji hasa wadogo wadogo ambapo wakulima na wafugaji hupata nafasi ya kubadilishana uzoefu katika shughuli zao za uzalishaji," alisema.
Alisema wafanyabiashara hutoa fursa nzuri ya kutangaza na kupanua soko la bidhaa zao hususan pembejeo na zana mbalimbali za kilimo, ufugaji, uvuvi na mambo mengine na kwa kuzingatia Katiba ya TASO moja ya majukumu ya kazi zake ni kukuza na kuendeleza sekta hizo ikiwemo uzalishaji wa bidhaa za maliasili na hifadhi za mazingira. Moyo alisema moja ya mbinu kubwa ya chama hicho ya kuchangia maendeleo ya jamii yote ya Watanzania na kuwaandaa, kuratibu, kuendesha na kusimamia maonesho hayo na ili kuwezesha TASO itekeleze hayo.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa