Home » » Baregu aonya kuhusu Bunge Maalumu

Baregu aonya kuhusu Bunge Maalumu

Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Profesa Mwesiga Baregu amesema, Bunge maalumu lijao la Katiba linaweza kugeuka kituko iwapo wajumbe wake wataweka mbele masilahi ya vyama vya kisiasa na kuacha misingi ya kujenga taifa moja na lenye mshikamano.
Pia amesema, pamoja na Tume hiyo ya Mabadiliko ya Katiba kukamilisha kazi yake lakini kwa upande mwingine hatakubali kukaa kimya pindi atakapoona kazi nzuri iliyofanywa ya ukusanyaji maoni ya wananchi ikidhihakiwa.
“Sitaweza kukaa kimya eti kwa sababu Tume imemaliza kazi yake huku nikiona watu wanapindisha mambo na kukebehi kazi nzuri ya Tume,” alisema.
Akizungumza kwenye kongamano lilipewa jina,“Katiba moja kwa Watanzania wote-Pamoja tutafika,” Prof Baregu alisema bila kuweka utashi wa kujenga taifa moja, Bunge lijalo linaweza kutawaliwa na vituko.
“Iwapo wajumbe watakwenda kwenye Bunge la Katiba huku wakiwa na ushabiki wa vyama vyao mimi naona kutakuwa na vituko vikubwa.Tunapaswa kutambua kwamba tunakwenda kutengeneza Katiba ya Taifa na siyo kwa kuegemea masilahi ya kundi fulani,” alisema.
Alisema itakuwa siyo jambo la busara kuona wajumbe wakielekea kwenye Bunge hilo huku wakiwa tayari wamevalia nguo rasmi za vyama vyao kwani kwa kufanya hivyo kunaweza kutia doa mchakato wa kupata Katiba Mpya.
Prof Baregu aliwataka wajumbe watakaokuwa kwenye Bunge lijalo kutumia lugha sahihi inayoeleweka kwa wananchi badala ya kuchanganya lugha kama inavyojitokeza sasa katika vikao mbalimbali vya Bunge.
Henzron Mwakagenda kutoka Jukwaa la Katiba alisema ufanisi wa bunge lijalo unatia mashaka.
“Sisi tulikuwa kwa kwanza kupinga suala la wabunge kuwa sehemu ya bunge hili na tulipinga pia Rais kuteua wajumbe. Inavyoonekana sasa Bunge hili lijalo huenda lisiwe na tija,tunakusudia kuandaa kongamano maalumu”.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa