Home » » Madalali feki wa BOT wanunua noti chakavu

Madalali feki wa BOT wanunua noti chakavu

Madalali feki wanaodai kutumiwa na Benki Kuu (BoT) wameibuka mitaani kununua noti chakavu za Tanzania na fedha za kigeni.
 
Baadhi ya madalali hao  wanapita vituo na kwenye majumba ya watu  jijini Dar es Salaam, kutangaza kuwa wananunua noti chakavu na kuzinunua kutoka kwa watu hasa wenye uelewa mdogo.
 
Wateja wanamiminika na kulipwa nusu ya thamani ya fedha walizotoa kwa  wanunuzi hao, ambao wakipokea noti ya  10,000 wanawapa Sh  5,000, kadhalika kwa Sh. 5,000 wanapewa 2,500 hivyo kupoteza nusu ya malipo waliyostahili.
 
Wateja hao walifika kwenye ofisi za NIPASHE Jumapili kutoa malalamiko ya kupunjwa, kuibiwa fedha zao na kutaja namba ya dalali mmoja mwenye namba 0656-105110, aliyetajwa kwa jina la Justine Mkomwa kuwa ni miongoni mwa watu wanaonufaika na   biashara hiyo maeneo tofauti jijini Dar es Salaam.
 
Hata hivyo, walisema mara nyingi wanakutana naye Buguruni kituo cha daladala kinachotizamana na  kituo cha  mafuta.
 
Wateja hao walidai  madalali wanaonunua fedha hizo wanawapunja  wanapowaletea fedha za kigeni hasa Yuro na Dola, ambazo kwa vile wengi hawajui hulipwa chini ya thamani ya nusu ya fedha wanayodanganywa kuwa wangepewa.
 
“Wananunua hata fedha za Kenya, Uganda, Oman  na Rial ya Yemen,” alisema  mteja ambaye  hakupenda jina litajwe.
 
Katika  mahojiano zaidi walibainisha kuwa madalali hao wa Buguruni wananunua fedha hizo na kudai kuwa wanashirikiana na vigogo wa BoT ambao wanazichukua na kuzipeleka kwenye akaunti zao zilizoko nje ya nchi.
 
Walisema vigogo hao wamewapa karatasi maalumu za kuunganisha na kutengeneza noti zilizochakaa  kabla ya kuwafikishia ili zisiendelee kuchakaa. 
 
Walidai kuwa awali wauza noti hao walikuwa wanajichanganya na wauza chenji za sarafu maeneo ya mengi jijini, hasa Mwenge lakini walifukuzwa katika kituo hicho.
 
Ilielezwa pia kuwa biashara hiyo imesambaa mikoani hasa Moshi na Arusha ambapo madalali hao wanauza na kununua bila kificho.
 
Alipohojiwa iwapo raia wanaweza kununua fedha  kwani kiutaratibu fedha chakavu hurudishwa kwenye mabenki au BoT, Naibu Waziri wa Fedha,  Mwigulu Nchemba, alisema biashara hiyo hairuhusiwi  kufanywa na madalali.
 
Walieleza pia noti chakavu inaporudishwa benki haipungui thamani  kama alifikisha Sh 10,000 anapewa noti mpya yenye thamani hiyo.
 
Alisema biashara hiyo ya madalali  ni haramu na kuahidi kuviagiza vyombo vya dola kuwasaka wahusika na kusisitiza:
"Hatujawahi kuweka wakala wa kununua fedha mitaani, wala noti  chakavu hazinunuliwi bali zinarudishwa benki au BoT, hilo ni kosa nipe muda nitaongea na vyombo vya dola ili wahusika wakamatwe," alisema.
 
Pamoja na maelezo hayo ya Waziri, watoa taarifa hao walisema fedha hizo ambazo hununuliwa kwenye vituo vya daladala na mitaani ni biashara ya ‘bingo’ inayozalisha faida ya kati ya sh. 150,000 na 300,000 kwa wiki.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa