Home » » Mchungaji: Hofu ya Mungu itawale

Mchungaji: Hofu ya Mungu itawale

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

MCHUNGAJI wa Kituo cha Nyumba ya Maombi, kilichopo Tabata Segerea, Dar es Salaam, Patrick Emmanuel amewataka wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kutanguliza hofu ya Mungu katika kipindi chote cha kujadili Rasimu ya Katiba.

Alisema kama wajumbe watakosa hofu ya Mungu, Watanzania wasitegemee kupata Katiba bora ambayo wataitumia kwa miaka 50 ijayo badala yake kutakuwa na malumbano yasiyo na tija ndani ya Bunge hilo.
Mchungaji Emmanuel aliyasema hayo mwishoni mwa wiki katika Kongamano Maalumu lililoandaliwa na kanisa hilo ili kuombea amani itawale katika Bunge hilo na Uchaguzi Mkuu ambao utafanyika mwaka ujao.
"Nimepata maono ya kuombea amani ya kitaifa ndani ya nchi yetu hasa ukizingatia kuwa, tuna mchakato mkubwa wa kupata Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu ujao, hivyo lazima tuwe na hofu ya Mungu katika kipindi hiki," alisema.
Aliwataka wajumbe wote waliopata fursa ya kuingia katika Bunge hilo, wasitafute umaarufu wa kuongea, bali wafanye kazi iliyowapeleka ili mwisho wa siku Taifa na wananchi wake wapate tumaini jipya kupitia katiba hiyo.
Alisema kama wajumbe wataacha kufanya kile wanachokihitaji Watanzania, Mungu atawaadhibu kwa sababu wananchi watakuwa na manung'uniko hivyo wao watapa adhabu.
"Hatutaki kuona damu ikimwagika katika Taifa hili kutokana na watu wachache ambao wametofautiana kwa sababu ya itikadi ya vyama au siasa ndio maana watumishi wa Mungu wanafanya kazi ya kuliombea Taifa usiku na mchana," alisisitiza.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Segerea, Azuri Mwambagi alisema umefika wakati wa viongozi wa dini kusimama kwa dhati kuliombea Taifa ambalo lina rasilimali za kutosha lakini zinatafunwa na watu wachache.
Alisema vijana wengi wamepoteza matumaini hasa wanapoona viongozi wachache wanatumia rasilimali za nchi kujinufaisha; hivyo ipo hatari ya kuvunjika amani iliyopo.
Kongamano hilo pia lilishirikisha watumishi mbalimbali kutoka nchi za Zambia na Namibia.

Chanzo;majira

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa