Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amesema Tanzania imeshuka kwa nafasi 
tisa katika orodha ya nchi zinazofanya biashara duniani zilizopo kwenye 
viwango vya Benki ya Dunia (WB) na kwa sasa inashika nafasi ya 145 kati 
ya nchi 189.
                
              
Akizungumza juzi katika  Uzinduzi wa Ripoti ya 
Mapitio ya Sera ya Uwekezaji nchini, Waziri Pinda alisema Tanzania 
inaweza kunufaika katika uwekezaji kama itatekeleza kikamilifu mapitio 
ya Mfumo wa Uwekezaji yaliyowasilishwa na Taasisi ya Ushirikiano wa 
Kiuchumi na Maendeleo (OECD) katika Ripoti ya Mapitio  ya Sera ya 
Uwekezaji.
“Ripoti inaonyesha Tanzania imeshuka nafasi tisa 
na inaeleza maeneo yenye changamoto na kuchangia kushuka kwa ufanyaji wa
 biashara ambao ni pamoja na upatikanaji wa mikopo, rushwa, vibali, 
biashara mipakani, ulipaji kodi na usajiliwa ardhi na mali,” alisema 
Pinda.
Katika hotuba yake Pinda aliwataka watendaji wa 
Serikali kupitia kwa kina mapitio ya ripoti hiyo na kutumia mapendekezo 
yake ili kufikia malengo ya uwekezaji yaliyowekwa katika Mpango wa 
Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Alifafanua kuwa ili kukabiliana na changamoto 
hizo, Serikali imeanzisha kituo katika Bandari ya Dar es Salaam ili 
kuondoa vikwazo katika barabara kubwa na kurahisisha ulipaji kodi.
Alisema malengo ya mapitio ya ripoti hiyo ni 
kuboresha hali ya uwekezaji na biashara nchini ambayo matokeo yake 
yatasaidia kuongeza wawekezaji.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
 
 
 
0 comments:
Post a Comment