Home » » TMA kubadili mbinu utoaji taarifa

TMA kubadili mbinu utoaji taarifa

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dk Agness Kijazi amesema licha ya mamlaka hiyo kutoa taarifa za hali ya hewa,   watumiaji wamekuwa hawazingatii  hali inayosababisha kuendelea kutokea kwa majanga.
Dk Kijazi alisema zipo sababu mbalimbali zinazochangia kutozingatiwa kwa taarifa hizo, ikiwamo namna zinavyotolewa huku watu wengine wakifikiri haziwahusu.
Kutokana na changamoto hiyo, TMA kwa kushirikiana na Serikali ya Norway imekuja na mpango wa utoaji taarifa za hali ya hewa kulingana na mahitaji ya watumiaji.
Katika mpango huo, Norway imetoa dola 10 milioni za Marekani kwa Tanzania na Malawi, ambazo zitatumika kuhakikisha utoaji taarifa za hali ya hewa unafanyika kwa ufanisi ili kuepukana na majanga.
“Huwa tunatoa taarifa lakini watumiaji wanashindwa kuzifutilia,  huenda ni kutokana na jinsi ambavyo zinatolewa matokeo yake tunakumbana na changamoto mbalimbali za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi,” alisema Dk Kijazi na kuongeza:
“Hivyo Shirika la Hali ya Hewa Duniani, limekuja na mpango huu kuhakikisha tunatoa taarifa sahihi kwa wakati mwafaka kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.”
Alisema kupitia mpango huo, taarifa za mamlaka hiyo zitasaidia nchi kuepukana na majanga mbalimbali yakiwamo ukame, njaa na kuhakikisha kunakuwapo  upatikanaji chakula salama.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Usafirishaji  na Miundombinu, Edwin Mujwahuzi alishukuru Serikali ya Norway kwa kuleta mpango huo ambao utasaidia kwa kiwango kikubwa  kuboresha huduma za hali ya hewa nchini.
Mujwahuzi alisema mamlaka hiyo ina changamoto mbalimbali, hivyo kujitokeza wafadhili wa aina hiyo kutasaidia kukabiliana nazo.
Alisema hivi sasa dunia ina mabadiliko makubwa ya teknolojia na kwamba, bado Tanzania haijapata vifaa vya kisasa kukabiliana na changamoto hizo.
Mujwahuzi alisema malalamiko ambayo yamekuwa yakielekezwa kwa mamlaka hiyo na wananchi, inatokana na kutokuwa na uelewa jinsi inavyokumbana na changamoto kwenye utendaji wake.
Aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa kufuatilia taarifa zinazotolewa, ili kuepuka majanga.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa