Home » » Ngeleja: Mjadala wa katiba usiwe wa Serikali tatu tu

Ngeleja: Mjadala wa katiba usiwe wa Serikali tatu tu

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, William Ngeleja akizungumza katika moja ya mikutano yake. 

Mwenyekiti Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na  Utawala, William Ngeleja, amewataka wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, wasijikite katika kujadili suala la muundo wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano tu, bali waangalie pia masuala mengine yanayogusa masilahi ya nchi.
Bunge Maalumu la Katiba linatarajia kuanza vikao vyake Februari 18 mwaka huu, mjini Dodoma na linatazamiwa kukaa kwa siku 70.
Ngeleja, ambaye  pia ni Mbunge wa Sengerema (CCM), alisema jana kuwa wajumbe wanapaswa kuangalia masilahi ya wananchi.
Alisema Tanzania inaundwa na wakulima, wafanyakazi, wavuvi na wafugaji na kwamba itakuwa busara kama Katiba Mpya, itakidhi mahitaji ya  makundi haya.
“Nchi yetu ina makundi mengi, sasa itakuwa vizuri kama Katiba Mpya itazingatia watu wote. Ila inasikitisha kuona watu wamejikita zaidi katika suala la muundo wa Serikali ya Muungano na kusahau mambo mengine,” aliongeza Ngeleja.
Hata hivyo, alikiri kuwa suala la muundo wa Serikali ya Muungano ni la muhimu lakini alisema haina maana kuwa masuala mengine yaachwe.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilitoa Rasimu ya pili ya Katiba inayopendekeza muundo wa Muungano wa Serikali tatu.
Ngeleja pia aliwataka wajumbe watakaojadili katiba kwenye Bunge la Katiba kuhakikisha kuwa Katiba Mpya inaangalia namna rasilimali za taifa zinavyoweza kumsaidia mwananchi wa kawaida.
“Nchi yetu imejaaliwa kuwa na rasilimali nyingi lakini  tatizo kubwa ni kuwa zimeshindwa kumnufaisha mwananchi wa kawaida,” alisema Ngeleja, ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini.
Alitaja rasilimali kama gesi, madini na mbuga za  wanyama kuwa ni mifano ya rasimali za taifa ambazo hata hivyo, haziwanufaishi wananchi wa kawaida.
Hali kadhalika alisema litakuwa jambo zuri ikiwa katiba ijayo  itaainisha namna viongozi watakavyosimamia rasilimali za nchi na kuhakikisha kuwa zinamnufaisha kila mmoja.
Alisema itakuwa jambo zuri zaidi ikiwa Katiba Mpya  itajikita zaidi katika kuweka msisitizo kwa Serikali kufanya kazi kwa uwazi zaidi na kusimamia masilahi ya watu.
Ngeleja, ambaye pamoja na kupongeza uteuzi uliofanywa na Rais Kikwete wa wajumbe 201 wa Bunge Maalumu la Katiba, pia aliwasihi wajumbe kuweka pembeni itikadi zao na  kuweka mbele masilahi ya wananchi.
Alishauri wajumbe hao kuhakikisha kuwa wanaendesha mijadala kwa utulivu, hekima na busara.
“Hatutarajii kuwepo kwa jazba wakati wa mijadala ya katiba. Wajumbe wanapaswa kuhakikisha kuwa wanajenga hoja zenye nguvu badala ya kulazimisha mambo yao,” alisisitiza Ngeleja.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa