Home » » vijana nchini waache kushiriki kwenye siasa?

vijana nchini waache kushiriki kwenye siasa?

Mfumo wa vyama vingi vya siasa ni hali ya kuwa na chama zaidi ya kimoja katika nchi moja. Madhumuni ya mfumo huu ni kupanua uwanja wa demokrasia kwa wananchi na kuleta ushindani wa kisiasa unaosaidia ukuaji wa demokrasia, uwajibikaji na kuleta maendeleo kwa nchi husika, ukiruhusu kuwapo chama tawala au muungano wa vyama hivyo pamoja na upinzani.
Hapa Tanzania mfumo huo ulirejeshwa mwaka 1992 na baadaye mwaka 1995 kufanyika Uchaguzi Mkuu kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.
Uchaguzi mwingine kwa mfumo huo umefanyika mwaka 2000, 2005 na mwaka 2010, ambapo viongozi wa vyama vya siasa wamekuwa wakinadi sera za vyama vyao kwenye kampeni na kutoa ahadi mbalimbali.
Hata hivyo sehemu kubwa wananchi, hasa vijana wamekuwa wakiambulia patupu kutoka kwa wagombea waliotoa ahadi kutaka kuchaguliwa katika nafasi za uongozi ikiwamo, udiwani, ubunge hata urais, baada ya wagombea husika kutangazwa washindi.
Wanasiasa wamekuwa wakiwatumia vijana kwa njia mbalimbali wakilenga kutimiza malengo yao kisiasa na kupata wanachotarajia, mwishowe kundi hilo la vijana ambalo ni nguvu kazi ya taifa huishia kuona wengine wakifaidi mafanikio huku wao kiendelea kubaki juani.
Kutokana na hali hiyo, uwanja wetu wa Sauti za Vijana uliwauliza: Wanazungumziaje ushiriki wao katika siasa nchini hasa wakati wa uchaguzi na manufaa wanayoyapata baada ya uchaguzi kumalizika?
Vijana hao walijibu ifuatavyo:
Gabriel Majaliwa (28):
Vijana tumekuwa tukitumika vibaya, bila hata mafanikio. Mbaya zaidi hao wanaowatumia, wamekuwa hawatekelezi yale waliyokuwa wakiwaahidi kwenye harakati zao za kutaka kuaingia madarakani. Nawashauri waachane na siasa.
Ramadhani Mwekwa (29):
Kwa taifa lolote linalohitaji mabadiliko, lazima vijana wawe mstari wa mbele kwani wao ndiyo kila kitu, hivyo mimi sioni ubaya wanapoungana na vyama wanavyovipenda wenyewe katika kudai au kupigania  mabadiliko.
Shija  Tumain:
Mada hii imekuja muda mwafaka, kwani vijana wanatakiwa kujifunza kuachana na masuala ya siasa kwani wamekuwa wakitumia muda mwingi kuwatengenezea maisha wengine, lakini wao wanaendelea kusota na ugumu wa maisha. Nawashauri wabadilike na kuchukua hatua zaidi.
Sophia Philimon (36):
Hata siku moja vijana hawawezi kukombolewa na siasa, lakini wanasiasa wenyewe wanatakiwa kuacha kuwatumia vijana kwa maslahi binafsi.
Wanawatembeza na kuwalaza njaa kwa ahadi nyingi, lakini mwishowe hakuna anayewajua tena.
Abeid Jonathan (31):
Acha vijana waendelee kutumika na wanasiasa kwani si Chadema wala CCM walioonyesha dhamira ya kweli ya kuwasaidia. Mfano; mwaka 2010 CCM iliwaahidi vijana ajira nyingi, lakini ajira hizo ziko wapi?
Chadema nao wanasema wakiingia madarakani watahakikisha wanatengeneza ajira kibao, huu wote ni uongo,  hivyo vijana wanatakiwa kujitambua
Maxmillian  Nangoa (28):
Ukiangalia vikundi vya ulinzi CCM, CUF au Chadema, wengi ni vijana lakini je, wananufaika vipi?
Wengi wao wanadanganyika kwa fedha kidogo, lakini sasa umefika wakati  vijana wakatambua thamani yao na kwamba wanatumika vibaya, mwisho wa siku wanajeruhiwa hata kupoteza maisha na hakuna wa kuwatetea.
Godfrey Mponjole (25):
Vijana wamekuwa wakifuata mkumbo, badala ya kuona madhara wanayoyapata katika harakati za siasa. Kubwa zaidi, wanapotezewa muda na hakuna anayewatimizia malengo yao. Nawashauri watambue kuwa wanasiasa sio watu wa kuwategemeza kuwatimizia ndoto zao.

Hamza Gawale (37):
Kwa siku za hivi karibuni, wazee wetu wameonekana  kupewa kisogo na vyama hivi kutokana na kutokuwa na nguvu za kushirika katika mikutano mingi, vijana bila kutambua kuwa wanapoteza muda, wamejikita katika siasa wakiamini CCM ikiondoka madarakani watapata unafuu na maendeleo. Hiyo ni ndoto isiyowezi kutimizwa na chama chochote cha siasa.
Deo Msambaki (25):
Madhara wanayopata vijana kutokana na siasa ni makubwa, wanakamatwa na kuwekwa mahabusu, wanapigana wao kwa wao na wengine wanapoteza maisha. Lakini ambao wanawapigania siku wakiingia madarakani hususan bungeni unasikia wanavyoongezeana posho. Unajiuliza; hivi wanawatetea vijana au wao na familia zao? Tuache kudanganyika tufanye kazi.
Kashaija Johnson:
Mimi naona ni bora nguvu wanazotumia vijana katika siasa wangezielekeza nyanja nyingine mfano; michezo, kuna uwezekano ingewafikisha mbali vijana kwani eneo hilo hakuna bugudha kama siasa inayotawaliwa na ura
Valentine  John :Wacha vijana wenyewe watumike kuwanufaisha wengine kwani fursa za kupata maendeleo ni nyingi. Mfano; inawezekana wakulima wakijiunga vikundi na kuanzisha mradi wa kilimo, hapo nina hakika utawafikisha mbali, lakini kwa kuwa wanapenda kuandamana juani bila faida yeyote.Waendelee na siasa, lakini watambue kuwa wanasiasa hawawezi kuwaletea mabadiliko yoyote.
Swali la wiki ijayo litakuwa:
Mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanaonekana kuwaathiri  vijana wengi hasa  kimaadili. Je, nini kifanyike ili  wasiendelee kuathirika zaidi?
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa