Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kimetangaza mgogoro na Serikali
kwa kushindwa kufanyia kazi madai mbalimbali ya walimu yanayofikia Sh61
bilioni, yakiwamo malimbikizo ya mishahara na likizo za walimu. Madai
mengine ni Serikali kutokufanya maandalizi mazuri ya mfumo wa kutathmini
utendaji wa walimu kwa lengo la kuwapandisha madaraja.
Rais wa CWT, Gratian Mukoba alisema juzi kwamba
chama hicho kimefikia uamuzi huo baada ya kuona kuwa katika madai hayo
matatu hakuna hata moja lililofanyiwa kazi na Serikali ambayo amesema
imekuwa ikitoa ahadi za uongo. Kwa mujibu wa kiongozi huyo, Baraza la
Taifa la CWT lilikutana Januari 27 hadi 29 mwaka huu na kuazimia kwamba
kero hizo za walimu ziwe zimepatiwa ufumbuzi mwishoni mwa mwezi
uliopita, vinginevyo chama hicho kitangaze mgogoro na Serikali.
Hizi siyo habari njema hata kidogo kwani uzoefu
umetuonyesha kuwa, kila itokeapo migogoro na mikwaruzano kati ya walimu
na Serikali, wanafunzi na wazazi wao ndio huwa majeruhi wa kwanza.
Katika hali kama hiyo, tumeshuhudia mara nyingi Serikali ikitoa machozi
ya mamba ikijifanya kuguswa pale inapolalamikiwa na wananchi kwa
kusababisha walimu kususia masomo na wanafunzi kukosa walimu wa
kuwafundisha.
Hivyo, mgogoro huo uliotangazwa na CWT unaashiria
balaa kubwa la uwezekano wa kutokea mgomo wa walimu nchi nzima. Kama
tulivyosema hapo juu, watakaoumia ni wanafunzi na wazazi wao na si
viongozi serikalini wanaotunga sera ambazo zinaonekana kuwakandamiza
walimu na taaluma yao. Tunasema hivyo kutokana na Serikali
kutoshughulikia kero za muda mrefu za walimu.
Kwa nini Serikali inakataa kusikiliza vilio vya
walimu? Moja ya sababu zinazotajwa kusababisha hali hiyo ni madai kwamba
viongozi wanapeleka watoto wao kusoma nje ya nchi, huku watoto wa
wananchi maskini wakisoma katika ‘shule’ zisizokuwa na madarasa,
madawati, walimu wala vifaa vyenye ubora. Kudidimia kwa viwango vya
elimu katika ngazi zote za elimu na kutokuwapo mfumo wa elimu endelevu
ni kielelezo tosha cha kuwapo hali hiyo.
Ndiyo maana tunapata wakati mgumu kuelewa sababu
zinazoifanya Serikali kutoona umuhimu wa kutafuta suluhisho la kudumu la
madai ya walimu. Inashangaza kuona kwamba Serikali iliiahidi CWT kwamba
mwezi uliopita ingelipa madai ya walimu yanayohusu malimbikizo ya
mishahara, lakini imebadili ahadi hiyo na kusema italipa fedha hizo
taratibu. Pamoja na vikao vingi vya majadiliano vilivyofanyika kutokana
na maagizo ya Mahakama ya Kazi ya mwaka 2012, hakuna chochote
kilichopatikana kutoka serikalini.
Serikali pia imeshindwa kupandisha walimu madaraja
kwa kasi iliyotarajiwa. Hadi mwezi uliopita ni baadhi ya wilaya katika
mikoa 12 ambako walimu wamepandishwa madaraja. Hii ni kwa sababu
Serikali haikufanya maandalizi mazuri ya kuweka mfumo wa kutathmini
utendaji kazi, hivyo kazi ya tathmini ya kupandisha walimu madaraja
kuchelewa.
Majadiliano ya mishahara ya walimu yalitokana na
mgomo wa walimu wa mwaka 2012, wakati Serikali ilikubali kulipa deni
hilo na kuandaa utaratibu wa kupandisha walimu madaraja. Sasa miaka
miwili imepita. Ndiyo maana tunaiona kauli ya Waziri wa Elimu na
Mafunzo, Dk. Shukuru Kawambwa kuwa Serikali inaendelea kujadiliana na
taasisi za fedha juu ya namna ya kulipa deni hilo, kuwa ni ulaghai
usiohitajika katika kushughulikia matatizo nyeti kama hayo.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment