Home » » Siri anguko la elimu hii hapa

Siri anguko la elimu hii hapa

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WANAFUNZI wanaosoma darasa la saba katika shule za msingi zilizofanya vibaya kwenye matokeo ya mwaka jana na kushika nafasi za mwisho wilayani Tunduru, wamesema hali hiyo inachangiwa na wazazi kuwashinikiza wajaze majibu ya uongo kwenye mitihani yao ya mwisho, ili wafeli kwa lengo la kuwanusuru na mkono wa sheria iwapo watafaulu na kushindwa kuwapeleka sekondari.
Wanafunzi hao walitoa kauli hiyo mbele ya Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, mkoani Ruvuma, Chande Nalicho, alipofanya ziara ya kushtukiza ili kujionea hali ya ufundishaji katika Shule za Msingi za Machemba na Mbatamila ambazo zilifanya vibaya kwenye mtihani wa darasa la saba.
Baadhi ya wanafunzi hao walimwambia mkuu wa wilaya kuwa chanzo cha wao kufeli mitihani ni wazazi na walezi.
Baadhi ya wanafunzi hao, Alli Machemba, Amina Mohamedi, walielekeza lawama zao kwa wazazi wao wakidai wanawashinikiza wajibu majibu ya uongo ili kuwanusuru na mkono wa sheria.
"Chanzo cha kufanya vibaya katika matokeo hayo ni wazazi na walezi wetu," alisisitiza mmoja wa wanafunzi hao na kuongeza kuwa inapotokea wanafunzi wakafeli wazazi hao huwafanyia sherehe kwa lengo la kuwapongeza.
Akitoa ushuhuda wa matukio hayo aliyekuwa Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Machemba, Namkanda Alli, alikiri kuwa hali hiyo ipo na kwamba ni moja ya sababu iliyomfanya aamue kuachia nafasi ya ukuu wa shule kutokana na kukosa ushirikiano kutoka kwa wazazi na walezi.
Alisema mwaka 2012 katika shule hiyo alifaulisha wanafunzi 35, lakini alijikuta akiachia nafasi hiyo kutokana na kukosa ushirikiano kutoka kwa wazazi na walezi, kwani wakati mwingine walimkejeli.
"Nilichukua uamuzi wa kuachia madaraka hayo ili nirudi darasani ili niondokane na masimango hayo," alisema Alli na kuongeza; " Wazazi na walezi walikuwa wakinifuata na kunihoji kwanini najifanya mwalimu bora."
Diwani wa Kata ya Kidodoma, Seif Yusiph, pamoja na kikundi cha vijana sita waliohitimu shahada ya kwanza katika Chuo Kikuu cha Dodoma wanazunguka kwenye kata za wilaya hiyo kuhamasisha wazazi na wanafunzi ili watambue umuhimu wa elimu.
Wahitimu wa shahada hiyo ya kwanza wanaozunguka na diwani huyo, ni Musa Lionga, Rashid Mapunda, Mariam Mtelela, Geres Mbena, Gaibu Rashid.
Walisema sababu zinazotolewa na wazazi hao si za kweli isipokuwa ni kutaka kuwaangamiza watoto wao kimaisha. Walisema haiwezekani mzazi aseme hana uwezo wa kulipa ada ya sh.20,000 kwa mwaka, wakati kila mwaka wanaongeza wake.
Kwa upande wa Mtawala wa Jadi wa kabila ya Wayao (Sultani Mataka wa 16) alilaani wazazi wanaohamasisha watoto hao kufeli mitihani yao ili kuwanusuru sheria isichukue mkondo wake.
Awali akitoa taarifa ya maendeleo ya taaluma katika Shule ya Msingi Machemba, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Ramji Mbawala, alisema shule yake ilifaulisha watoto wote katika matokeo ya mwaka 2013.
Kwa matokeo hayo alisema shule hiyo ilishika nafasi ya 133 kati ya 137 zilizopo wilayani humo.
Akizungumzia hali hiyo kwa niaba ya Ofisa Elimu Shule za Msingi wilayani humo, Christantusi Haule, alisema visingizio vinavyotolewa na wazazi havina ukweli wowote.
Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Nalicho alikemea tabia ya utoro uliokithiri miongoni mwa wanafunzi pamoja na wazazi ambao hawachukui hatua zozote kwa watoto wao wanapofanya vibaya.
"Kuanzia sasa ni marufuku wazazi kuwafanyia sherehe wanafunzi wanaofeli," alisisitiza Nalicho na kuongeza kuwa mtu atakayekaidi agizo hilo sheria itafuata mkondo wake.
Alisema hata wakifanya kwa kificho watagundulika tu kwa vile Serikali ina mkono mrefu.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa