Home » » ZITTO AHIMIZA MIFUKO YA JAMII KUSAIDIA SEKTA ZIISIZO RASMI

ZITTO AHIMIZA MIFUKO YA JAMII KUSAIDIA SEKTA ZIISIZO RASMI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Sera ya Maendeleo ya Hifadhi ya jamii isipofanyiwa mikakati ya kujumuisha sekta sizizo rasmi nchini umaskini utaendelea kuwa mwiba mchungu na janga la kitaifa katika siku za usoni.
Takwimu mbalimbali zinaonyesha kuwa Watanzania wengi wapo kwenye sekta isiyo rasmi. Takribani asilimia 70 wapo kwenye ukulima mdogo na asilimia 10 wamejiajiri kwenye shughuli mbalimbali kama biashara ndogondogo, madini, sanaa, michezo na uchuuzi mwingine.
Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa ya mwaka 2013 inaonyesha kuwa wanachama wa mifuko yote ya hifadhi ya jamii nchini ni takribani 1.1 milioni hivyo ni dhahiri kuwa hifadhi ya jamii inawahusu watu wachache ambao ni sawa na asilimia sita ya nguvu kazi na asilimia tatu ya Watanzania wote.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe alisema kuwa kundi kubwa la wananchi hawachangii katika kapu la pensheni kwa sasa hii ikiwa na maana kwamba mzigo huo ni mkubwa na usiokwepeka kwa taifa pindi idadi ya wazee itakapoongezeka katika kipindi cha miaka michache ijayo.
“Hili ni janga la taifa…tusifumbwe na muundo wetu wa idadi ya watu hivi sasa ambapo zaidi ya nusu ya Watanzania wana umri chini ya miaka 18 na asilimia 72 wana umri chini ya miaka 30. Hili kundi la watoto linaweza kuwa gawio iwapo tutajipanga vizuri,” alisema Kabwe na kuongeza;
“Tusipojipanga hili ni bomu ambalo likilipuka tutatafutana. Ipo siku itafika ambapo hili kundi la watoto halitakuwa na uwezo wa kufanya kazi tena lakini itabidi livishwe na kulishwa.”
Mwenyekiti huyo ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini alisema lazima Serikali ihakikishe kuwa hifadhi ya jamii inahusisha watu wengi zaidi kwa kuwaandikisha katika sekta isiyo rasmi na hasa wakulima na wafugaji, wavuvi na wachimbaji madini, wafanya biashara ndogondogo na wengineo.
Alisema huko ndiko kwa kuelekea ikiwa inahitajika Tanzania imara, bora na yenye neema huku akitoa angalizo kuwa suala hilo linahitaji utashi wa uamuzi makini.
Akitolea mfano wa nchi ambazo zimechukua hatua hiyo kiongozi huyo alisema nchi kama Korea ya Kusini, Thailand na China.
“Nchi ya China imepata mafanikio makubwa kwa kufikisha hifadhi ya jamii kwa wakulima vijijini. Serikali za nchi hizo zimeshirikiana na mifuko ya hifadhi ya jamii kuhakikisha raia wao wengi wanapata ulinzi wa kijamii ili kupambana na umaskini,” alibainisha Kabwe.
Hata hivyo Kabwe alisema Tanzania ilijaribu kufanya hivyo katika Jimbo la Kigoma Kaskazini ambapo wakulima 750 wa kahawa kupitia Chama cha Ushirika cha Msingi kiitwacho Rumako walijiunga na NSSF mwaka 2013 Machi lakini bado nguvu na jitihada zaidi zinahitajika.
 Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa