Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Wabunge wa Jiji la Dar es Salaam, Iddi Azzan (Kinondoni) na Abas
Mtemvu (Temeke) wameitaka Serikali ikusanye kodi ya pango katika jiji
hilo ili kuongeza mapato yake na kuachana na utamaduni wa kutegemea
mapato katika soda, bia, sigara na vinywaji vikali.
Wakizungumza wakati wa kuchangia mjadala wa Bajeti
Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2014/15 juzi jioni, wabunge hao pia
waliponda ujenzi wa barabara za mabasi yaendayo kasi, wakidai kuwa ni
nyembamba na hazikidhi viwango.
“Kodi ya pango ikikusanywa Dar es Salaam kwa mwezi
Serikali inaweza kupata Sh600 bilioni. Kama kweli tunataka mapato
tuamue maana kuna nyumba zinakodishwa kwa mwezi Sh3 milioni,” alisema
Azzan.
“Vitendo vya uhalifu vilivyokithiri Dar es Salaam
kwa sasa vinatokana na Serikali kutokuwa na fedha za kutosha kwa ajili
ya kuwalipa askari, sambamba na kuwajengea nyumba, sasa jeshi
limezidiwa. Kusanyeni kodi ipasavyo,” alisema Azzan.
Mbunge huyo aliiponda bajeti hiyo na kuifananisha
na bajeti za miaka ya sitini kwa maelezo kuwa haina kitu kipya na kwamba
watendaji wa Serikali walioiandaa ni mizigo.
“Nitashangaa sasa Serikali ikikabidhiwa barabara
za mabasi yaendayo kasi na ikapokea, barabara hizi ni nyembemba na
sehemu ya watembea kwa miguu ni ndogo mno. Watu wanatumia saa mbili
kutoka majumbani mwao hadi ofisini, barabara za jiji hili ni mzigo,”
alisema.
Akichangia mjadala huo Mtemvu ameitaka Serikali
kukopa fedha ili kulinusuru jiji hilo kwa kuweka flyovers (barabara za
juu)), “Hatuwezi kupata maendeleo stahiki kama watu wanatumia saa mbili
kutoka majumbani mwao kwenda kazini.”
Alifafanua kuwa kutojengwa kwa ghati namba tatu na
mbili katika Bandari ya Dar es Salaam kunaikosesha mapato Serikali
kutokana na meli kukaa kati ya wiki mbili hadi tatu, zikisubiri kushusha
mizigo.
Chanzo:Mwananchi
Chanzo:Mwananchi
0 comments:
Post a Comment