Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » POLISI WAOMBA RADHI KWA WAHARIRI

POLISI WAOMBA RADHI KWA WAHARIRI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, imewaomba radhi Mkurugenzi wa Kampuni ya The Guardian, Bw. Kiondo Mshana na Mhariri wa Gazeti la Nipashe, Bw. Jesse Kwayu.

Kamishna Msaidizi wa Polisi ambaye pia ni Mkuu wa Upelelezi wa kanda hiyo, Jafari Mohamed aliomba radhi hiyo jana baada ya jeshi hilo kuwa andikia barua Bw. Mshana na Bw. Kwayu likiwataka wafike Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi kwa ajili ya mahojiano.

Katika barua ya jeshi hilo iliyoandikwa Julai 21, mwaka huu, jeshi hilo lilidai mahojiano hayo yangehusu habari iliyoandikwa na gazeti la Nipashe, Julai 8 mwaka huu, ukurasa wa kwanza ikiwahusisha polisi wa kikosi cha pikipiki kuomba na kupokea rushwa.

"Tunawaomba radhi Bw. Mshana, Bw. Kwayu pamoja na Wahariri wote wa vyombo vya habari nchini kwa usumbufu uliojitokeza kwani jeshi halikufuata taratibu zinazopaswa badala yake tuliandika barua ya kuwaita Kituo Kikuu kwa mahojiano kuhusu habari hii.

"Hakuna jalada lolote la kesi ambalo limefunguliwa dhidi ya viongozi hawa ila tulikuwa tukihitaji msaada wao ili tuweze kuwabaini Polisi wanaojihusisha na rushwa," alisema Mohamed.

Aliongeza kuwa, yeye kama Kamishna  wa jeshi hilo, hakuwa akifahamu kama Msaidizi wake Mrakibu wa Polisi (SSP), Amani Makanyaga, amewaita Wahariri hao ofisini kwake kwa barua.

"Nawaombeni radhi kwa hilo kwani si lazima kila kitu kinachofanyika, bosi akifahamu hasa kikiwa cha kawaida lakini kwa hili la msaidizi wangu kuwaita bila kunijulisha, limenishtua na kukiri amepotoka," alisema.

Alisema SSP Makanyaga alipaswa kuwatafuta Wahariri hao kwani ni wadau muhimu ili waweze kumpa ushirikiano wa kuwapata Polisi wanaotumia nafasi zao kulichafua jeshi hilo.

"Kimsingi sisi hatuna ugomvi na vyombo vya habari kwani niwadau wetu wakubwa wa kufichua maovu...nitafanya mazungumzo na hawa Wahariri ili tuweze kulifuatilia suala hili," alisema.

Hata hivyo, SSP Makanyaga alikiri kosa hilo na kuwaomba radhi Wahariri akiwaomba waendelee kushirikiana kwani barua aliyoiandika imetafsiriwa vibaya na tayari kuna askari waliohojiwa na wanaendelea kukusanya malalamiko kutoka kwa wadau wengine na wananchi.

"Lengo langu la kuwaandikia barua viongozi hawa si kuwashtaki ila ni kupata msaada kutoka kwao tuweze kuwabaini askari wengine wenye tabia ya kuomba na kuchukua rushwa," alisema.

Kwa upande wake, Bw. Mshana alisema ipo haja ya  askari polisi kupewa mafunzo ambayo yatahusu namna ya kufanya kazi na vyombo vya habari ili kuacha kujikuta wakiita watu wasiohusika kuwahoji.

"Mimi kama Mkurugenzi ni Mtendaji ndani ya chumba cha habari lakini sihusiki kuandaa gazeti hivyo kuniita kuhojiwa ni kunipotezea muda wa kutekeleza majukumu yangu kikazi...najitolea kutoa mafunzo kwa vijana wa jeshi hili ili waweze kufahamu namna ya kufanyakazi na vyombo vya habari," alisema.

Naye Bw. Kwayu aliungana na Bw. Mshana akisema kitendo kilichofanywa na SSP Makanyaga kinaonesha ni namna gani ana uelewa mdogo kiutendaji.

Katika habari iliyoandikwa na gazeti hilo, ilielezea jinsi askari hao walivyozigeuza pikipiki walizopewa kuwa nyenzo za kukusanya pesa bila huruma na walivyojigeuza kuwa askari wa usalama barabarani na kuvizia malori.

Habari hiyo iliongeza kuwa, askari hao wamekuwa kero jijini Dar es Salaam wakiacha kutekeleza jukumu lao la kupambana na uhalifu na kujiingiza katika vitendo vya kukamata magari na kudai rushwa

Chanzo:Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa