Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MWENYEKITI wa Baraza la
Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA), Bw.John Heche,
ametangaza kutogombea tena nafasi hiyo katika uchaguzi uliopangwa
kufanyika Septemba 10, mwaka huu kutokana na umri wake kuwa mkubwa.
Akizungumza na
waandishi wa habari Dar es Salaam, Bw.Heche alisema anaheshimu Katiba ya
chama hicho ambapo kutokana na umri wake kuvuka miaka 30, hatagombea
tena nafasi hiyo.
Alisema uchaguzi wa
mwaka huu utasimamiwa na waangalizi wengine kutoka nchi mbalimbali
wataalikwa kutokana na BAVICHA kujenga mahusiano mazuri na vijana kutoka
nchi nyingi za Ulaya.
"Kwa sasa nina umri wa
miaka 32, kikatiba na mwongozo wa chama chetu, siwezi kugombea na mimi
naheshimu hilo lakini tumefanya mambo mengi kwani chama ni vijana na
sisi tumehakikisha kuanzia ngazi ya shina, matawi, kata,wilaya na jimbo
tumeweka viongozi hivyo tupo imara kuanzia ngazi ya chini," alisema.
Aliongeza kuwa,
uchaguzi wa mwaka huu watausimamia kikamilifu kwa kuondoa vibaraka wote
wanaoendeshwa kwa 'rimoti' na wale ambao itabainika wametoa rushwa ili
kupata uongozi, watachunguzwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na
Rushwa nchini (TAKUKURU).
"Hatupo tayari kuona
uchaguzi unafanyika katika mazingira ya rushwa na watu wasio na sifa
kuongoza baraza hili kwani uchaguzi uliopita ulitawaliwa na vurugu
kubwa," alisema Bw. Heche.
Kwa upande wake, Katibu
Mkuu wa BAVICHA, Bw. Deogratias Munishi, alisema hadi sasa baraza hilo
limeunda misingi zaidi ya 250 na matawi 19,000 nchi nzima.
Aliongeza kuwa, hadi
kufikia Agosti 15, mwaka huu ngazi za majimbo na wilaya zinapaswa
kukamilisha chaguzi zake na Agosti 30, mwaka huu ngazi zote za mikoa
ziwe zimefanya chaguzi zake zote.
"Nami natangaza rasmi
kuwa umri wangu hauniruhusu kugombea tena Ukatibu Mkuu hivyo
sitagombea...kuanzia Agosti 10-25, mwaka huu ni muda wa kuchukua na
kujaza fomu za kugombea nafasi za uongozi ndani ya baraza ngazi ya
Taifa.
"Uchaguzi wa mwaka huu
unawahusu vijana wote waliozaliwa Januari mwaka 1984 si chini ya hapo,
nafasi zinazogombewa ngazi ya majimbo, Wilaya na Mkoani Mwenyekiti,
Katibu,Mratibu Muhamasishaji na Mweka Hazina," alisema Bw. Munishi.
Alisema ngazi ya Taifa
ni Mwenyekiti Taifa, Makamu Mweyekiti Bara na Zanzibar, Katibu Mkuu na
Manaibu Makatibu Wakuu kutoka Zanzibar na Bara, Mratibu Mhamasishaji
Taifa na Mweka Hazina.
Nafasi zingine ngazi ya
Taifa ni wajumbe watano wa kuwakilisha vijana kwenye Baraza Kuu la
Chama hicho wanne kutoka Tanzania Bara na mmoja Zanzibar, wajumbe 20 wa
kuwakilisha vijana katika Mkutano Mkuu wa chama hicho ambapo wajumbe 15
watatoka Tanzania Bara na watano kutoka Zanzibar.
Naibu Katibu Mkuu wa
baraza hilo kutoka Tanzania Bara, Bi. Ester Dassi, naye ametangaza rasmi
kutogombea nafasi hiyo kutokana na umri wake kuwa mkubwa hivyo
amewataka wanawake wajitokeze kugombea nafasi hizo
Chanzo:Majira
0 comments:
Post a Comment