Home » » JK ATEUA MAJAJI 20 MAHAKAMA KUU

JK ATEUA MAJAJI 20 MAHAKAMA KUU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mjumbe  wa Sekretarieti ya  Bunge la Katiba, Jaji Mteule Leila Mgonya, akikata keki iliyoandaliwa na Kamati  Namba moja ya  Bunge la hilo baada ya kuteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania . wanaoshuhudia wajumbe wa Kamati hiyo, kutoka kushoto  ni  Ally Keissy,  Martha Mlata na Umi Mwalimu

Rais Jakaya Kikwete amemteua Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP), Eliezer Feleshi kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Feleshi ameteuliwa pamoja na wengine 19 kushika wadhifa huo akiwamo Naibu Mkurugenzi Mkuu, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru ), Lilian Mashaka na wataapishwa leo Ikulu.
Uteuzi huo umepongezwa na Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Charles Rwechungura akisema Serikali imesikiliza kilio chao cha muda mrefu cha kutatua tatizo la upungufu wa majaji nchini.
“Tunaipongeza Serikali kwa kutusikiliza ingawa si kwa asilimia 100.”
Mara ya mwisho Rais Kikwete aliwateua majaji saba wa Mahakama Kuu ya Tanzania Juni 8, 2012. Majaji wengine walioteuliwa katika uteuzi mpya ulioanza Agosti 13, mwaka huu ni Penterine Kente ambaye alikuwa Msajili wa Mahakama ya Rufani na Benedict Mwingwa aliyekuwa Msajili wa Mahakama Kuu.
Wengine ni Edson Mkasimongwa ambaye alikuwa Katibu wa Jaji Mkuu, David Mrango aliyekuwa Msajili Baraza la Ushindani na Mohamed Gwae aliyekuwa Msajili Mahakama Kuu, Kitengo cha Kazi.
Dk John Ruhangisa aliyekuwa Msajili Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Firmin Matogoro aliyekuwa Naibu Mwenyekiti, Baraza la Rufaa la Kodi, Barke Sehel aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Winfrida Korosso aliyekuwa Katibu Mtendaji, Tume ya Kurekebisha Sheria, Leila Mgonya aliyekuwa Msaidizi wa Waziri Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu na Awadhi Mohamed ambaye alikuwa Mchunguzi Mkuu wa Takukuru.
Wengine ni waliokuwa mawakili wa kujitegemea, Lugano Mwandambo kutoka Kampuni ya Rex Attorneys, Amour Said Khamis wa Kampuni ya AKSA Attorneys na Dk Paul Kiwelu ambaye pia alikuwa Mhadhiri Mwandamizi, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT).
Wengine ni Rose Ebrahimu ambaye alikuwa wakili wa kujitegemea wa kampuni ya Bulyankulu Gold Mine Ltd, Salma Maghimbi aliyekuwa Mjumbe wa Tume ya Ushindani (FCC), Dk Mary Levira ambaye alikuwa Kaimu Mkuu wa Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu Kishiriki cha Ruaha na Dk Modesta Opiyo Makopolo aliyekuwa Mkuu wa Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu, Mzumbe.
Akizungumzia uteuzi huo, Dk Modesta alisema: “Nimejisikia furaha kwa kuniona na kutambua kwamba ninaweza na sitawaangusha. ”
Dk Kiwelu alisema: “Uadilifu ni changamoto kubwa ninawaomba wenzangu kuhakikisha haki inatendeka kwa kila mmoja na kuepuka kupindisha sheria”.
Sehel alisema: “Nitatumia nafasi yangu kuhakikisha haki inaendelea kutendeka na kusimamiwa ipasavyo.”
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa