Home » » WANAFUNZI WASHINDA ELIMU YA UWEKEZAJI

WANAFUNZI WASHINDA ELIMU YA UWEKEZAJI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

SHINDANO la elimu ya uwekezaji kwa wanazuoni kwa mwaka 2014, lililokuwa likiendeshwa na Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) limemalizika kwa kuwapata washindi watatu wa kwanza kutoka vyuo vikuu mbalimbali nchini.

Shindano hilo lililojulikana kama DSE Scholar Investment Challenge 2014 lilidhaminiwa na Benki ya NMB pamoja na Kampuni ya Mawasiliano ya Selcom na Mfuko wa kuendeleza sekta ya fedha (FSDT) lilimalizika Juni 2014.

Akizungumza katika hafla fupi ya kuwatambulisha washindi hao jana Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa soko la hisa Dar es Salaam, Moremi Marwa alisema kuwa, shindano hilo lilihusisha zaidi ya wanafunzi 5,000 kutoka vyuo vya elimu ya juu kote nchini.

Marwa aliwatangaza washindi hao kuwa ni Dynko Amosi (SUA) ambae ndiye mshindi wa kwanza na kupewa kitita cha sh.1,000,000, mshindi wa pili akiwa ni George Firimin (IFM) na kupewa zawadi ya sh.600,000 na mshindi wa tatu akiwa ni Godlove Kelly(UDSM) ambae alipewa zawadi ya sh.400,000.

Aliongeza kuwa, shindano hilo ni kampeni endelevu ya kila mwaka inayowalenga vijana wa kitanzania walioko kwenye vyuo vya elimu ya juu nchini ili kufanikisha dhana ya kutoa elimu juu ya uwekezaji katika taasisi za kifedha.

"Katika shindano hili kila mshiriki hupewa mtaji wa kuanzia ili kuwaweka kwenye soko la hisa kwa kipindi cha miezi mitatu,"alisema.

Alisema kuwa, nia kubwa ya kampeni hiyo ni kuwafundisha na kuwahamasisha vijana kujenga tabia ya kuwekeza na kutunza fedha kwa kuonesha kwa vitendo sababu na namna ya kununua na kuuza dhamana kwenye soko la hisa.

Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya njia mbadala wa Benki ya NMB, George Kivaria alisema kuwa nia ya benki hiyo ni kuona inafanikisha malengo ya kutoa elimu kwa vijana juu ya namna ya uwekaji akiba kwenye taasisi za kifedha.

Aliongeza kuwa, huu ndio muda wa kuondoa ile dhana potofu ya kuwa wanaowekeza kwenye soko la hisa ni watu wenye uwezo tu.

"Katika soko la hisa kila Mtanzania anaweza kuwekeza, sio kwa wale wenye uwezo tu hisa zipo za bei tofauti tofauti hivyo kila Mtanzania anaweza kumudu kununua hisa," alisema.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa