
Kamati Ndogo ya Maadili ya CCM leo inaketi 
kutoa hatima ya makada wa chama hicho waliotajwa kuhusika katika kashfa 
ya Akaunti ya Tegeta Escrow.
                
              
Kikao hicho kitakuwa chini ya Makamu Mwenyekiti wa
 CCM - Bara, Philip Mangula kama ilivyoagizwa na Kamati ya CCM 
iliyokutana wiki iliyopita.
Walioitwa katika kamati hiyo ni aliyekuwa Waziri 
wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka ambaye 
ni mjumbe wa Halmashauri Mkuu (NEC) na Kamati Kuu ya CCM (CC) pamoja na 
wajumbe wa NEC, Andrew Chenge (Mbunge wa Bariadi Magharibi) na William 
Ngeleja (Sengerema).
Kwa kuwa uamuzi wa CC unasisitiza utekelezaji wa 
maazimio ya Bunge, kwa vyovyote unamlenga pia Waziri wa Nishati na 
Madini, Profesa Sospeter Muhongo ambaye mpaka sasa amewekwa kiporo.
Kamati Kuu iliyofanyika Januari 13, mwaka huu 
Zanzibar iliazimia kuwa hatua za kimaadili zichukuliwe kwa wote 
waliohusika na ukiukwaji wa maadili kwenye sakata la Escrow ambao wako 
kwenye vikao vya uamuzi vya CCM.
Pia kikao hicho kiliitaka Serikali kuendelea 
kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu sakata hilo ambalo lilikiweka chama 
hicho katika wakati mgumu katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 
uliomalizika hivi karibuni.
Kutokana na azimio hilo, Ngeleja, Profesa 
Tibaijuka na Chenge wanakabiliwa na adhabu ya kuvuliwa nyadhifa 
walizonazo ndani ya vikao vya amuzi vya CCM.
Makada hao walitajwa bungeni kuwa walipokea 
mamilioni ya shilingi kutoka katika akaunti ya VIP Engineering 
inayomilikiwa na James Rugemalira. Chenge na Profesa Tibaijuka walipokea
 Sh1.6 bilioni wakati Ngeleja alipokea Sh40.4 milioni.
Hata hivyo, Ngeleja anayetajwa kutaka kuwania 
urais anaweza kukumbwa na adhabu nyingine iwapo atabainika kuwa 
alikwenda kinyume na adhabu aliyopewa pamoja na wenzake watano ya 
kuhusishwa na ukiukwaji wa maadili kwenye mchakato wa kutaka kuteuliwa 
na chama hicho kugombea nafasi hiyo.
Adhabu hiyo aliyopewa Ngeleja pamoja na Waziri 
Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, 
January Makamba, Bernard Membe na Stephen Wasira inamalizika Februari 
mwaka huu na baada ya hapo itafanyika tathimini kuona kama walizingatia 
masharti ya adhabu zao.
Kwa mujibu wa taarifa ya CC, ambao hawakuzingatia masharti wataongezewa adhabu.
Tayari uteuzi wa Profesa Tibaijuka umeshatenguliwa
 na sasa Rais Kikwete anasubiriwa kumtangaza mrithi wake na kumalizia 
‘kiporo’ cha Profesa Muhongo.
Maazimio ya Bunge
Azimio la pili la Bunge lilitaka Waziri wa Nishati
 na Madini, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mwanasheria 
Mkuu wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini na Wajumbe 
wa Bodi ya Wakurugenzi wa Tanesco wawajibishwe, kwa kuishauri mamlaka 
yao ya uteuzi kutengua uteuzi wao.
Kati ya hao wote, mtu pekee ambaye mpaka sasa bado hajachukuliwa hatua yoyote ni Profesa Muhongo.
Jaji Frederick Werema ameshajiuzulu nafasi yake ya
 Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Eliakim Maswi aliyekuwa Katibu Mkuu wa 
Wizara ya Nishati na Madini alisimamishwa kazi na Bodi ya Tanesco 
imeshaundwa mpya.
Bunge pia liliazimia kuwa Chenge na Ngeleja ambao 
walikuwa wenyeviti wa kamati za Bajeti na ile ya Katiba, Sheria na 
Utawala, mtawalia, kuvuliwa nyadhifa zao, jambo ambalo bado linasuasua.
Sakata la Escrow pia linaweza kuwaathiri wanasiasa
 hao kwa upande mwingine kwa kuwa wote bado wana nia ya kutetea nafasi 
zao za ubunge katika majimbo yao.
Chanzo:Mwananchi
Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
0 comments:
Post a Comment