Home » » TFF, POLISI WADHIBITI VURUGU VIWANJANI

TFF, POLISI WADHIBITI VURUGU VIWANJANI

Siku zote Watanzania tunafahamu kuwa soka ni mchezo unaopendwa na mashabiki wengi siyo katika ardhi yetu pekee bali kote ulimwenguni.
Hakuna shaka kwamba ushabiki na mapenzi hayo ya soka vinaonekana kwa watu ambao wamekuwa wakijikamua na hivyo kulipa viingilio na kisha kuingia katika viwanja mbalimbali ili kushuhudia mechi mbalimbali.
Ushahidi upo wazi wa jinsi ambavyo soka inavyopendwa na vijana kwa wazee na kwa ufupi ni mchezo ambao hauna rika, haujali kipato cha mtu.
Kwa bahati mbaya, soka katika nchi yetu imekuwa ikichezwa na wakati mwingine kukumbwa na matukio ambayo hayapendezi wala kuvutia, yakiwamo ya vurugu zinazotokea kwenye viwanja vyetu vingi.
Mechi za Ligi Daraja la Kwanza zinazoendelea katika viwanja mbalimbali nchini, ikiwamo mchezo wa Majimaji na Kurugenzi Mafinga kutoka Iringa zimekumbwa na vurugu kubwa baada ya timu hizo kumaliza kwa sare ya bao 1-1.
Tunakemea vitendo hivi vya utovu wa nidhamu ambavyo vimejitokeza kwenye mechi za ligi, ikiwamo michezo inayohusisha vyombo vya ulinzi na usalama, hususan timu zinazomilikiwa na Jeshi la Polisi. Timu hizo za Polisi Dodoma, Tabora na Mara zimetoa mfano na nidhamu mbaya baada ya kuhusika katika matukio ya vurugu nyingi ambako waamuzi wamepigwa na kuumizwa.
Tunajiuliza swali ambalo wasimamizi wa ligi, kwa maana ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Bodi ya Ligi lazima walijibu.
Je, wamejiandaa vipi katika kuwalinda waamuzi ambao wamekuwa wakishambuliwa, kuumizwa na wachezaji au mashabiki kwenye mechi ambazo zinahusisha timu za Polisi?
Kama sivyo, je, wamejiandaa vipi kukabiliana na matukio hayo maovu kwenye mechi ambazo timu hizo za Polisi zinawania kuingia Ligi Kuu?
Tunaishauri TFF na Bodi ya Ligi wachukue hatua zote zinazofaa ili kuzuia matukio hayo maovu kwenye viwanja vya soka yanayozidi kuota mizizi katika siku za karibuni.
Tunawashauri TFF lazima wachukue hatua, zikiwamo za kuhakikisha ulinzi unakuwa wa kutosha, hasa kwenye mechi za Polisi ambazo zina rekodi ya kufanyika vurugu kama ambazo imeshuhudiwa waamuzi kufanyiwa vitendo vya kikatili.
Ni wazi TFF na Bodi ya Ligi lazima wachukue hatua zikiwamo za kutoa adhabu kwa wahusika ambao wanachafua sifa za mchezo wa soka katika nchi yetu.
Tunasema, TFF waweke mikakati madhubuti ikiwezekana wakati wa mechi za ligi hiyo zinazohusisha polisi, watafute walinzi wakiwamo wa vyombo vingine vya ulinzi kama Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) ambao wanao polisi jeshi, yaani ‘Military Police’ ambao watasaidia kulinda amani na kudumisha amani kwenye viwanja.
Pia, tunalishauri Jeshi la Polisi lichukue hatua na kuwafunza askari wao namna ya kulinda amani kwenye viwanja vya soka kwa kuangalia wenzao wa Ulaya, ambao huingia kwenye viwanja siyo kama mashabiki, bali walinzi wanaotimiza wajibu wao.
Tunasema kuwa bado tuna imani kubwa kwa polisi wetu na tunaamini kuwa wanaiweza kazi yao, hivyo wasiache matukio ya vurugu viwanjani yawachafulie jina lao na kazi nzuri ambayo wanaifanya.
Tunaamini, polisi wetu hawajashindwa katika kazi hii ya kulinda na kudumisha amani kwenye viwanja vyote vya soka, tatizo ni kuwa hawako tayari kwa kazi hiyo ambayo ni nyeti, hata kama wao hawaoni umuhimu wake.
Chanzo:Mwananchi 
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa