Home » » KAMA PANYA ROAD WAMETUSHINDA BASI BALAA!

KAMA PANYA ROAD WAMETUSHINDA BASI BALAA!

Ilikuwa pata shika nguo kuchanika katika baadhi ya maeneo ya jiji hili wiki iliyopita baada ya kundi la vijana wanaojulikana kwa jina maarufu la ‘Panya Road’ kuzua vurugu, kuvamia maeneo ya biashara huku wengine wakiangusha vipigo kwa kila waliyekutana naye.
Watu walikuwa wanakimbia utadhani mambomu ya machozi yamerushwa. Wafanyabiashara walifunga biashara zao mapema tofauti na siku za kawaida ili kunusuru siyo tu mali zao bali hata maisha yao.
Mwenye ndugu jamaa au rafiki aliyekuwa maeneo hayo alipia simu au kumtumia ujumbe ili kumjulia hali kama yupo salama au ameshapitiwa na Panya Road. Siku ile ilikuwa kama filamu. Lakini kumbe ni vijana wadogo tu inawezekana kudhibitiwa.
Kama hiyo haitoshi ilidaiwa kuwa baadhi ya vijana wa kundi hilo baada ya kuona watu wengine wamefunga biashara zao na kukimbia kwa ajili ya usalama wao, walikuwa wanarukia kwenye magari yaliyokuwa yanatembea barabarani na kuvunja vioo vya magari. Watakachokutana nacho halali yao.
Hata hivyo jioni polisi walitoa ufafanuzi juu ya taharuki hiyo iliyokuwa imetokea na kusambaza na vyombo mbalimbali vya habari hapa nchini pamoja na mitandao ya kijamii. Kauli ya kiusema kuwa, Jeshi la Polisi lipo salama na kwamba watahakikisha amani inakuwepo na kwamba hao vijana hawawezi kulishinda Jeshi la Polisi.
Kauli hiyo nzito ilitoa matumaini. Angalau baada ya hapo watu walifarijika kidogo kuona kuwa polisi wanadhibiti hali hiyo. Kesho yake wakasema kuwa wamewakamata baadhi yao.
Haikuishia hapo, Jeshi la Polisi liliendelea na msako katika maeneo mbalimbali ya jiji hili. Vijana waliyokuwa wadhani kuwa ni wanachama wa kundi hilo walikuwa wanachukuliwa na polisi na kupelekwa kituoni kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
Nilishuhudia moja ya kamatakamata hiyo katika Kituo cha Daladala cha Segerea. Polisi walikuwa wanakamata kila kijana aliyekuwa amekaa bila shughuli yoyote. Kwa sababu inasemekana kuwa kundi hilo linaundwa na vijana wa mtaani, wavuta bangi na wasiokuwa na ajira. Kwa hiyo kijana aliyekuwa na mwonekana wa kuvaa ovyo hakusalimika.
Nilisikia kuna wale waliotoa kitu kidogo wakaachiwa. Sasa sijui kweli au ni maneno ya watu tu. Mimi na wewe hatufahamu. Nadhani mbinu nyingine inahitajika hapa.
Hata hivyo, lazima tujiulize mwaka jana kundi hili hili liliibuka na vuguru za namna hii. Mengi yalisemwa kuhusu kundi hilo na baada ya muda hali ilikuwa shwari. Ikasemekana kuwa waliibuka baada ya mwenzao kuuawa kutokana ana kufanya uhalifu.
Awamu hii tena inadaiwa kuwa walianzisha fujo hizo baada ya mwenzao kuuawa. Sasa kila mara hali hii imekuwa ikijitokeza kwa kundi hilo la vijana na watu wanaishi kwa wasiwasi.
Ni vyema tujiulize hivi hawa vijana ni kina nani, wanaishi wapi. Inawezekana ni wenzetu, ndugu zetu marafiki zetu lakini tunawanyamazia. Sidhani kama hatua madhubuti zikichukuliwa kundi dogo kama hili linaweza kushinda maelfu ya watu wa jiji hili. Tusisubiri hadi wao waibuke huko waliko na kufanya vurugu ndiyo na sisi tuanze kuwasaka.Tena kuwasaka huko huenda wakati mwingine kukawa kwa kubahatisha ili kuwaondoa wananchi hofu. Inawezekana wale waodhaniwa kuwa ni panya road siyo na wasiyodhani wapo wanasubiri hali iwe shwari waanzishe vurugu. Kama ndiyo hivyo tufuge ‘paka’ inawezekana hiyo ikawa dawa nzuri ya kumaliza tatizo hili.
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa