Home » » MIAKA 10 YA THT: KUTOKA UZALISHAJI WA VIPAJI VYA MUZIKI HADI UBUNIFU

MIAKA 10 YA THT: KUTOKA UZALISHAJI WA VIPAJI VYA MUZIKI HADI UBUNIFU

Mwanamuziki wa kundi la THT Lameck Ditto akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari. 

Kama umewahi kusikia kuhusu kituo cha Tanzania House of Talent (THT) na ukajua kwamba kinajishughulisha na uzalishaji wa vipaji vya sanaa ya muziki, hivi sasa kituo hicho kimetangaza mwelekeo mpya baada ya kutimiza miaka 10.
Shamra shamra hizo ambazo zimeanza kuadhimishwa wiki hii na zitafikia kilele Desemba mwaka huu, zimekuwa na lengo tofauti na ule wa awali ambapo sasa kituo hicho hakitapokea wanafunzi wa sanaa ya uimbaji na dansa na badala yake kitaegemea upande wa ubunifu wa mitindo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa maadhimisho hayo, Meneja Mkuu wa Kituo hicho, Mwita Mwaikenda alisema ni heshima kubwa kuweza kusherehekea miaka 10, wakiwa wamefanikisha mambo mengi makubwa.
Mwaikenda alisema kituo hicho kinatarajia kuadhimisha miaka 10 toka kuanzishwa kwake ifikapo Januari 30 mwaka huu, hafla itakayofanyika Escape 1 jijini Dar es Salaam.
THT iliyoanzishwa mwishoni mwa mwaka 2005 ilikuwa na lengo la kuwasaidia vijana wenye vipaji, lakini wasio na uwezo wa kujiendeleza wenyewe katika sekta mbalimbali za sanaa.
“Tulianzisha kituo hiki tukiwa hatuna chochote zaidi ya imani yetu kwa vijana walio na vipaji, tulianza hatuna chochote lakini leo tumesaidia vijana zaidi ya 3,000 waliopita katika kituo hiki kwa miaka 10, ambao wengi wao walikuwa ni watoto wa mitaani lakini leo wanajimudu wao na familia zao,” alisema Mwaikenda.
Akielezea kuhusu mwelekeo wa kituo baada ya miaka 10, Mwaikenda alisema anaamini kituo kimefanya kazi yake tayari kwa kuweza kuchagiza sanaa ya muziki nchini, na sasa ni wakati wa kuendelea kusaidia wadau au vituo vingine kama Mkubwa na Wanawe kufika THT ilipofika.
“Kimsingi mwaka huu ndiyo wa mwisho kuendela kupokea wanafunzi wapya wa kuimba, na mpango wetu ni kuendelea kukuza kituo kwa kuanzisha kampuni ya ushonaji na ubunifu wa nguo kwa kutumia kitenge ambao tunaamini utatoa ajira kwa vijana wengi zaidi hapa nchini,” alisisitiza Mwita.
Mwaikenda alisema kampuni ya ubunifu na ushonaji kwa kutumia vitenge, tayari ishaanza mchakato wake kwa kuhusisha wadau wa biashara ya vitenge na mbunifu mahiri Ally Remtullah, mwanamitindo Flaviana Matata wakiwa ndiyo walezi na wasimamizi wa mradi, ambao utaanza na wabunifu wanaochipukia Neyonce pamoja na Adam Mchomvu.
“Kwa kuanza mradi utapeleka wabunifu nchini China ili wakajifunze zaidi juu ya ubunifu na kuongeza ubora kwenye kazi zao, wakirudi tunaamini wataweza kuwafundisha vijana wengi zaidi na kutimiza lengo letu la kuwasaidia vijana kujiajiri,” alimaliza Mwita.
Meneja Masoko wa THT, Michael Nkya alisema kituo kililenga kusaidia watoto wa mitaani, lakini baadaye walijitokeza wengine waliokuwa na uwezo katika vipaji vyao lakini wanahitaji kuviendeleza na hatimaye kuingia katika shughuli za uratibu.
“Tulivyoanza si tulivyo sasa, kwani tunaratibu matamasha mbalimbali kama Fiesta, mkutano wa Smart Partnership, Sensa ya mwaka 2013, Sherehe za miaka 50 ya Muungano pamoja na mikutano, matamasha kadha wa kadha,” alisema.
Alisema THT imeendelea kukua kwa kuweza kuanzisha studio yake ambayo imeweza kurekodi matangazo, nyimbo za wasanii wote wa THT pamoja na wengine wengi kama ‘Mdogo Mdogo’ na ‘Number One Remix’ ya Diamond, ‘Me and You’ ya Ommy Dimpoz, ‘Prokoto’ ya Victoria Kimani na nyingine nyingi.
Nkya alisema kwa sasa THT inatengeneza vipindi mbalimbali vya televisheni kama 69 Records, na vingine vinavyorushwa chaneli za nje huku pia ikijivunia kuwa na maktaba ya nyimbo kubwa zaidi nchini.
“Shukrani zetu za dhati kwa kweli ni kwa Serikali, hasa hasa Mheshimiwa Rais Kikwete, ambaye toka mwanzo alikubali wazo na akaamini muziki unahitaji elimu ya peke yake, pia kampuni mbalimbali ambazo wamekuwa wakitupa kazi pamoja na vyombo vyote vya habari kwa kutuunga mkono siku zote,” alisema Nkya.
Kituo hicho kimezalisha wasanii wengi sambamba na dansa wakiwemo Mwasiti Almasi, Linah Sanga, Barnaba Elias, Mataluma, Marlaw, Recho, Amini, Kadja Nito, Dito na wengine wengi.
Chanzo:Mwananchi 
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa