Home » » USHINDANI UTATUWEKA MJINI- FM ACADEMIA

USHINDANI UTATUWEKA MJINI- FM ACADEMIA

Ilitosha kwa FM Academia kumweteka na umaarufu na uzoefu wao mkubwa kwenye soko la muziki wa dansi na kudharau bendi nyingine zinazojaribu kukaribiana nao, lakini haijavimba kichwa na badala yake inaheshimu wapinzani wao wote.
“Bila ya kuwapo washindani, hakuna ambaye angeweza kupima ubora wa bendi nyingine,” anasema kiongozi wa bendi hiyo inayojumuisha wasanii wengi wenye asili ya Kongo, Nyoshi El Saadat.
“Kama ilivyo kwa timu (za mpira) na hata wagombea, kwenye nafasi yoyote lazima kuwe na sababu ya kuwapo kwa ushindani, ndiyo anatambulika nani bora.”
Nyoshi alifafanua kuwa wao wameliona hilo na kila siku wanafanya kazi kupambana na ushindani uliopo sokoni na hata katika kumbi za burudani, ikiwa ni pamoja na kuangalia watu wanataka nini.
“Bendi za muziki wa dansi zipo nyingi, hasa zinazopiga kwa lengo la kuwateka vijana wapenda burudani, hivyo lugha ya taifa ya FM Academia ni muziki wenye kiwango kwanza , mengine baadae,” alisema mwimbaji huyo kiongozi wa FM Academia.
Bendi hiyo inakabiliwa na kibarua kigumu ya kushinda ushindani kutoka bendi kama African Stars, maarufu kwa mtindo wa Twanga Pepeta, Mashujaa, Malaika na Akudo Sound, ambazo pia zinajumuisha wasanii mchanganyiko kutoka Tanzania na Kongo.
FM ilianzishwa mwaka 1997 na kundi la wanamuziki kutoka FM Musica iliyokuwa chini ya Kampuni ya FM Bank ambao waliungana na wanamuziki wengine waliokuwa pamoja jijini Nairobi kwenye bendi ya Bogoss Musica.
Bendi hiyo imepata kutoa albamu 10 zilizopata mafanikio makubwa sokoni na kushinda tuzo za Kili Music Awards mara kadhaa.
Kwa mujibu wa Nyoshi, FM Academia kwa sasa inatamba na nyimbo kama “Fataki”, “Otilia”, “Ndoa ya Kisasa”, “Neema”, “Dai Chako Ulaumiwe”, “Maisha”, “Madudu”, “Miraessa” na “Intro” ambazo zitakuwa kwenye albamu mpya.
Nyoshi alielezea siri ya mafanikio kwa miaka 18, kuwa ni kuona mbele na kutambua mashabiki wanahitaji nini kwenye utitiri wa bendi za muziki wa dansi uliopo sasa.
Alisema kuwa hapingi kuwapo na bendi nyingi anafurahia kwani anaamini ni changamoto kwa viongozi na wamiliki wa bendi kuwa makini wakitambua kuna wanaowakimbiza wakitaka kuwapora tonge walilonalo mkononi.
Kiongozi huyo alisema kuwa haamini kuwa wingi wa bendi na muziki wa dansi kutopigwa redioni kunavunja umaarufu wa muziki huo.
Alisema kwa kawaida bendi mara nyingi huwa na mashabiki wake ambao hupelekeana habari wanapokwenda kwenye shoo, hivyo kazi ya bendi ni kuhakikisha mashabiki wanapoingia ukumbini wanapata wanachokitaka.
Alieleza kuwa mashabiki wakiburudika wanakuwa mabalozi wazuri kuutangaza muziki kwa kuomba nyimbo redioni na kwenye vituo vya runinga na wenye redio watalazimika kupiga ili kuwaridhisha wateja wao.
Alizitaja changamoto za kuendesha bendi ikiwamo kuhakikisha wanamuziki wanaridhika na kubaki kwenye bendi kwa muda mrefu.
“Siku za hivi karibuni imeingia tabia ya wanamuziki kupenda kuhamahama wakidhani watapata maslahi au wanaweza kuwa wanayapata kweli. Hali hiyo imekuwa ikiyumbisha bendi nyingi, hivyo changamoto kubwa ni kuwafanya waone umuhimu wa kubaki kwenye bendi yao, ” alisema Nyoshi
Chanzo:Mwananchi 
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa