Home » » NGELEJA,CHENGE WAPELEKWA MAADILI

NGELEJA,CHENGE WAPELEKWA MAADILI

Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za mitaa (LAAC) za Mitaa, Kangi Lugola akizungumza wakati wa kikao cha kamati hiyo kilichofanyika Dar es Salaam jana. Kushoto ni Mjumbe mwenzake, Omari Nundu.

 Licha ya Bunge kuazimia kuwa wenyeviti wa kamati zake waliotajwa kuhusika kwenye kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow wavuliwe nyadhifa zao, hali imekuwa tofauti katika vikao vya kamati hizo vilivyoanza jana baada ya baadhi yao kuongoza vikao hivyo. Jana, Kamati Kuu ya CCM imeamua viongozi hao, Andrew Chenge, William Ngeleja Na Profesa Anna Tibaijuka wafikishwe Kamati ya Maadili ya chama.
Awali, walitakiwa kuachia ngazi na kamati zao katika mabano ni Ngeleja (Katiba, Sheria na Utawala), Chenge (Bajeti) na Victor Mwambalaswa (Nishati na Madini).
Kikao cha 16 na 17 cha Bunge kiliazimia kuwa kamati husika za kudumu za Bunge zichukue hatua za haraka na kwa vyovyote vile kabla ya Mkutano wa 18 wa Bunge unaoanza Januari 27, kuwavua nyadhifa zao wenyeviti tajwa wa kamati husika.
Hata hivyo, jana, Ngeleja alisema anaendelea na madaraka yake, kwa kuwa hatua iliyopo sasa ni ya uchunguzi.
“Mimi naendelea na kazi zangu kama mwenyekiti wa kamati, najua uchunguzi wa suala hili bado unaendelea, baada ya hapo ikithibitika ndipo Bunge litachukua uamuzi nami sitakuwa na budi kutekeleza,” alisema Ngeleja.
Aliongeza: “Ingawa ninajua kuna shinikizo kwa baadhi ya watu kwa sababu wanazozijua wao hawapendi kutuona katika nafasi hizi.”
Kwa upande wake, Chenge alisema: “Sikuwahi kutangaza kujiondoa katika nafasi hii ya uenyekiti. Nimeshangaa taarifa zilizotolewa katika baadhi ya vyombo vya habari.”
Alisema tuhuma zinazomkabili hazimuumizi kichwa kwa sababu hazina ukweli, “Dhamira hainiumi kwa sababu siwezi kushiriki kuiba fedha za wananchi. Mimi ni kama tumbili hata hapa nitaruka.”
Makamu mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk Festus Limbu alisema suala la Chenge linasubiri uamuzi utakaotolewa na Spika wa Bunge, Anne Makinda. “Kamati imeamua kwa busara Chenge akae pembeni na makamu mwenyekiti aongoze vikao huku ikisubiri hatua atakazozichukua Spika (Makinda)...lakini siyo taarifa kwamba Chenge kajiuzulu, siyo kweli.”
“Unajua suala hili unaweza kusema bado ni bichi, Chenge ni mwenyekiti mteule wa Spika, lakini wenyeviti wengine wanachaguliwa na wajumbe wa kamati zao, labda Spika hajaona wa kumteua au anataka kuiachia kamati ifanye uchaguzi, hili litategemea na yeye,” alisema Limbu ambaye ni Mbunge wa Magu (CCM)
Kuhusu wafadhili wa maendeleo ambao kamati hiyo ilikutana nao jana alisema wametoa asilimia 50 ya Dola 558 milioni ambazo wahisani hao waliahidi.
Kikao cha Kamati ya Nishati na Madini kiliongozwa na Makamu mwenyekiti wake, Jerome Bwanausi ambaye alilithibitishia gazeti hili kwamba hawakufanya uchaguzi wowote.
Alipotafutwa kwa simu Mwabalaswa na kutakiwa kuzungumzia hatima yake, alijibu kuwa hawezi kuzungumzia suala hilo kwenye simu.
Mkurugenzi wa Idara ya Shughuli za Bunge, John Joel alisema: “Suala halipo kikanuni, bali ni maagizo yaliyotolewa na Bunge kwa hiyo mwenye nafasi nzuri ya kulizungumzia ni Spika.”
Hata hivyo, habari zilizopatikana jana usiku ndani ya Kamati Kuu ya CCM zilieleza kuwa, Ngeleja, Chenge pamoja na Profesa Tibaijuka suala lao imeachiwa Kamati ya Maadili ya CCM chini ya mwenyekiti wake, Philip Mangula.
Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa