Home » » WASHTAKIWA HAO KUTOKA TRA, TANESCO NA BOT WALISOMEWA

WASHTAKIWA HAO KUTOKA TRA, TANESCO NA BOT WALISOMEWA

Sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow jana liliendelea kuibua mapya baada ya vigogo watatu kutoka Benki Kuu (BoT), Mamlaka ya Mapato (TRA) na Shirika la Umeme (Tanesco) kufikishwa mahakamani wakikabiliwa na mashtaka ya kuomba na kupokea rushwa.
Kufikishwa mahakamani kwa watu hao watatu kunafanya jumla ya watu waliopandishwa kizimbani kufikia watano baada yaw engine wawili kutinga mahakamani mapema wiki hii.
Waliofikishwa Mahakama ya hakimu Mkazi wa Kisutu jana ni meneja misamaha ya kodi wa TRA, Kyabukoba Leonard Mutabingwa, mwanasheria mwandamizi wa Tanesco, Steven Roman Urassa na mkurugenzi wa fedha wa BoT, Julius  Rutta Angello, ambao wote kwa pamoja wanatuhumiwa kuomba na kupokea jumla ya Sh1.923 bilioni zinazohusishwa na fedha zilizokuwa Akaunti ya Tegeta Escrow.
Wote walisomewa mashtaka ya kuomba na kupokea rushwa ya mamilioni ya fedha kutoka akaunti hiyo, kinyume na kifungu cha 15 (1)(a) cha Sheria ya Kupambana na Rushwa Namba 11 ya Mwaka 2015. Walifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Janeth Kaluyenda na Devotha Kisoka
Mahakama ya Kisutu jana
Akisoma hati ya mashtaka katika kesi namba 16 ya 2015 dhidi ya Kyabukoba, mwendesha mashtaka wa Takukuru, Leonard Swai alidai mbele ya Hakimu Kaluyenda kuwa Januari 27, 2014 katika Benki ya Mkombozi wilayani Ilala , alipokea Sh1.6 bilioni kupitia akaunti namba 00110202613801.
Swai alidai  kuwa fedha hizo ni  sehemu ya fedha za Akaunti ya Tegeta Escrow na kwamba alipewa na James Burchard Rugemalira, ambaye ni mshauri wa kitaalam, mkurugenzi wa kampuni ya VIP Engineering na mkurugenzi wa zamani wa IPTL. Alisema alipewa fedha hizo kama tuzo kwa kuiwakilisha mahakamani kampuni ya Mabibo Beer, Wines and Spirits ambayo ni mali  ya Rugemalira, kitu ambacho ni kinyume cha sheria.
Alidai kuwa Julai 15, 2015, Kyabukoba akiwa benki hiyo ya Mkombozi alipokea rushwa ya Sh161.7 milioni, Agosti 26,2014 alipokea tena rushwa ya Sh 161.7 milioni na  Novemba 14, 2014 alijipatia Sh161.7 milioni kupitia kwenye akaunti hiyo, ikiwa ni tuzo kwa kuiwakilisha kampuni hiyo ya  Rugemalira.
Kyabukoba alikana mashtaka hayo na upande wa mashtaka ulidai upelelezi wa kesi hiyo umeshakamilika na akaomba ipangiwe tarehe nyingine kwa ajili ya mshtakiwa huyo kusomewa maelezo ya awali (PH).
Pia aliiomba mahakama kuzuia akaunti inayodaiwa kutumika kuchota fedha hizo kwa muda hadi hapo kesi ya msingi itakapoamuliwa na kutolewa uamuzi, ombi ambalo Hakimu Kaluyenda alikubaliana nalo.
Hakimu Kaluyenda alimtaka mshtakiwa huyo kuwa na wadhamini watatu wanaoaminika na wawili kati yao wawe watumishi kutoka taasisi inayotambulika kisheria na mwingine awe na barua inayoaminika na pia kila mmoja kusaini hati ya dhamana ya maneno yenye thamani ya Sh340 milioni na kwa  upande wa mshtakiwa kutoa Sh1 bilioni taslimu ambayo ni nusu ya fedha anazodaiwa kupokea kama rushwa, au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo.
Pia alitazuiwa kutoka Dar es Salaam bila ya kuwa na kibali cha mahakama. Mshtakiwa huyo alishindwa kukamilisha masharti hayo na kupelekwa rumande hadi Januari 29, 2015, siku ambayo atasomewa maelezo ya awali (PH).
Katika kesi namba 15,2015, inayomkabili Angello wa BoT iliyokuwa mbele ya Hakimu Kisoka, ilidaiwa kuwa Februari 6, 2014 katika benki hiyo, mtuhumiwa alipokea rushwa ya Sh161.7 milioni kupitia akaunti namba 00120102646201 ambazo aliomba na kupokea zikiwa sehemu ya fedha za escrow.
Swai alidai kuwa fedha hizo zilikuwa tuzo kwa kufanikisha malipo yaliyotolewa katika Akaunti ya Tegeta Escrow na fedha hizo kulipwa PAP, jambo ambalo lilikuwa ni kinyume na mwajiri wake.
Angello alikana mashtaka na upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na akaomba ipangiwe tarehe nyingine kwa ajili ya mshtakiwa huyo kusomewa maelezo ya awali, lakini akaomba mahakama pia izuie akaunti yake, maombi ambayo yalikubaliwa.
Hakimu Kisoka alimtaka mshtakiwa huyo kuwa na wadhamini wawili wanaominika, mmoja kati yao awe mtumishi wa serikali  na kila mdhamini asaini dhamana ya Sh50 milioni, ikiwa ni masharti ya dhamana.
Pia alimtaka mshtakiwa huyo kutoa fedha taslimu Sh 80.8 milioni kiasi ambacho ni nusu ya fedha ambazo anatuhumiwa kupokea kutoka kwa Rugemarila ama hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo.
Hakimu Kisoka aliiahirisha kesi hiyo hadi Januari 27,2015 na mshtakiwa aliachiwa huru baada ya kukamilisha masharti ya dhamana.
Katika kesi namba 14/2015 inayomkabili Urassa wa Tanesco, Swai alidai kuwa Februari 14,2014 mshtakiwa huyo akiwa benki hiyo aliomba na kupokea rushwa ya Sh 161.7 milioni kutoka katika Akaunti ya Tegeta Escrow.
Swai alidai kuwa  siku hiyo, mshtakiwa huyo alipokea kiasi hicho kupitia akaunti  namba 00120102658101 na kwamba zilikuwa sehemu ya fedha za escrow zilizotoka kwa Rugemalira, ikiwa ni tuzo kwa kuiwakilisha Tanesco na kampuni nyingine iliyoingia nayo mkataba mahakamani.
Kama ilivyokuwa kwa wengine, Swai alidai kuwa upelelezi umekamilika, na hivyo mshtakiwa atasomewa maelezo ya awali Februari 11
Hakimu Kaluyenda aliyeisikiliza kesi hiyo pia, alimtaka mshtakiwa huyo kuwa na wadhamini  wawili wanaoaminika  na mshtakiwa awasilishe Sh81 milioni taslimu mahakamani mahakamani hapo ama mali isiyohamisha yenye thamani hiyo.  Mshtakiwa huyo alitimiza masharti.
Kashfa hiyo ya Akaunti ya Tegeta Escrow iliyoibuliwa na Bunge iliitikisa nchi na hadi sasa imesababisha Profesa Anna Tibaijuka kuvuliwa uwaziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kutokana na kuingiziwa Sh1.6 bilioni na Rugemarila.
Pia, aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema alijiuzulu kwa maelezo kuwa ushauri wake kuhusu kodi iliyotakiwa kukatwa kwenye fedha hizo, haukueleweka na badala yake ulizua tafrani.
Pia katibu mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliachim Maswi amesimamishwa kazi kwa uchunguzi.
Katika uamuzi wake, Bunge liliagiza watuhumiwa wote wa kashfa hiyo, akiwamo Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, ambaye bado ameachwa kiporo na Rais Jakaya Kikwete, na wenyeviti wa kamati za Bunge za kisekta wawajibishwe.
Hao ni pamoja na Andrew Chenge anayeongoza Kamati ya Bunge ya Bajeti aliyedaiwa kupokea Sh1.6 bilioni kutoka akaunti hiyo.
Pia, William Ngeleja (Kamati ya Sheria na Katiba) aliyepokea fedha, Victor Mwambalaswa (Nishati na Madini), ambaye pia alikuwa mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi Tanesco.
Hali kadhalika, tayari watumishi kadhaa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wamesimamishwa kutokana na kashfa hiyo
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa