Na Fatma Salum- MAELEZO, Dodoma.
Serikali
imewahakikishia wananchi kuwa inaendelea na utekelezaji wa mpango wa
ujenzi wa zahanati kila kijiji, vituo vya afya kila kata na Hospitali
katika kila Wilaya ikiwa ni mkakati wake wa kuboresha huduma za afya
kote nchini.
Hayo
yamesemwa leo bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala
za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Suleiman Jafo wakati
akijibu swali la Mbunge wa Busokelo Mhe. Fredy Mwakibete kuhusu Mpango
wa kujenga zahanati kila Kijiji na kituo cha afya kila Kata.
Mhe.
Jafo alisema kuwa Serikali kwa kushirikisha nguvu za wananchi
inaendelea na ujenzi wa zahanati, vituo vya afya na Hospitali kila
Wilaya ambapo ujenzi huo unafanyika chini ya Mpango wa Maendeleo ya Afya
ya Msingi (MMAM).
“Utekelezaji
wa Mpango huo unaendelea na kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017
Halmashauri zimetengewa shilingi bilioni 182.5 kwa ajili ya utekelezaji
wa miradi ya afya na kipaumbele kitatolewa katika kukamilisha miradi
viporo badala ya kuanzisha miradi mpya.” alisema Jafo.
Kwa
mujibu wa Mhe. Jafo, Ofisi ya Rais TAMISEMI inafanya tathmini ya
utekelezaji wa mpango wa MMAM ili kujua idadi ya Vijiji ambavyo havina
zahanati, Kata ambazo hazina vituo vya afya na Wilaya ambazo hazina
Hospitali lengo likiwa ni kuhakikisha maeneo hayo yanapewa kipaumbele na
kutengewa fedha ili kusogeza huduma za afya karibu na wananchi.
Akieleza
mafanikio ya mpango wa MMAM, Mhe. Jafo alisema kuwa chini ya mpango huo
vituo vya kutolea huduma za afya vimeongezeka kutoka 5,255 mwaka
2006/2007 hadi 6,935 mwaka 2014/2015 sawa na ongezeko la asilimia 39.9
hivyo kuna matumaini makubwa ya kuvifikia vijiji vingi kupitia mpango
huo.
0 comments:
Post a Comment