| Jiwe la Msingi linaloashiria ujenzi wa Kijiji cha Wasanii Wilayani Mkuranga lililowekwa wakati wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2014 Wilayani Mkuranga. |
| Baadhi ya Wasanii pamoja na Wanakijiji wakifuatilia hafla ya uwagawaji maeneo kwa ajili ya wasanii na Mwanasoka bora wa ndani ya Afrika, Bw. Mbwana Samatta 5 Juni, 2016 Wilayani Mkuranga. |
| Mzee Mbwana Samatta akiishukuru Serikali kwa msaada aliopewa mwanae Mbwana Samatta kwa kupewa eneo la ukubwa wa ekari tano 5 Juni, 2016 Wilayani Mkuranga. |
| Msanii wa masuala ya Abstract Painting, Bw. Faridu Mathias Taratib akiishukuru Serikali kwa niaba ya Wasanii wenzie kwa kupewa maeneo ya kuendeleza kijiji cha Wasanii 5 Juni, 2016 Wilayani Mkuranga. |
![]() |
| Baadhi ya nyumba katika kijiji cha Wasaanii kama zinavyoonekana katika picha Wilayani Mkuranga. |
(PICHA ZOTE NA BENEDICT LIWENGA, MAELEZO)
NA BENEDICT LIWENGA, MAELEZO.
WASANII
nchini wamehimizwa kuchangamkia fursa ya kujiunga na Shirikisho la Wasanii
Tanzania (SHIWATA) ambao ndiyo waanzilishi wa kijiji maalum cha wasanii
kilichopo Wilayani Mkuranga, lengo likiwa kuwavutia wasanii hao kuhamia katika
kijiji hicho.
Kauli hiyo
imetolewa jana na Kaimu Mkurugenzi Idara ya Sanaa, Wizara ya Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo, Bi. Leah Kihimbi wakati wa hafla maalum ya kuwakabidhi maeneo
wasanii 35 akiwemo Mwanasoka Mahiri wa Tanzania anayechezea soka la Kulipwa
nchini Ubelgiji Bw. Mbwana Samata.
Bi. Kihimbi
amewapongeza baadhi ya wasanii wa Shirikisho hilo kwa uthubutu wao wa kujiunga
ndani ya kijiji hicho na kupata nafasi ya kujengewa makazi yao.
Katika hafla hiyo, wasanii mbalimbali nchini wamefanikiwa kupewa vyeti vya umiliki wa maeneo yao waliyogawiwa kulingana na pesa za michango yao katika Shirikisho lao huku akiwataka wasanii wengine kuiga mfano huo.
"Nimeambiwa
kuwa Shirikisho hili la SHIWATA linafanya kazi zake kwa kuwashirikisha wadau
wake kama vile kufanya warsha, makongamano, mafunzo ya kitaaluma na
ujasiriamali, kwahiyo naamini kijiji hiki kitasheheni sifa zote hizi",
alisema Kihimbi.
Akizungumzia
suala la miradi miwili katika eneo hilo, alisema kuwa SHIWATA imechagua eneo
zuri huku akiahidi kuzifikisha kwa Waziri mwenye dhamana katika Wizara yake,
Mhe. Nape Nnauye baadhi ya changamoto zilizopo ndani ya eneo hilo kama vile
barabara, maji pamoja na umeme ili wasanii wasipatwe na sumbufu wowote pindi
wanapohamia kijijini hapo.
"Nimeambiwa
kuwa huku kuna Miradi miwili ya ekari 500 katika kijiji cha Ngarambe ambayo ni
mashamba makubwa pamoja na ekari 300 ambazo ndo hizi tulizopo hapa, naipongeza
Halmashauri ya Mkuranga kwa jambo hili zuri na kwakweli SHIWATA katika hili hawajafanya
makosa kuchagua eneo hili, niwaahidi kuwa nitazifikisha baadhi ya changamoto mlizoniambia
katika eneo hili kwa Mhe. Waziri kwani yeye anapenda sana kuona maendeleo
katika tasnia hii", alisema Kihimbi.
Kwa upande
wake Afisa Utamaduni Wilaya ya Mkuranga Bw. Pembe Mlekwa alieleza kuwa, Wilaya
yake imekuwa ikifanya jitihada za kuwawezesha wasanii kupatiwa maeneo hayo wakati
wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2014 lengo likiwa kuitambulisha Tanzania na
Dunia kwa ujumla.
"Lengo
la Wilaya yetu la kutenga maeneo haya ni kuitambulisha Tanzania na Dunia kwa
ujumla kuwa kuna kijiji cha Wasanii hapa nchini, kama ilivyo kule kwa wenzetu
kama vile Hollywood nchini Marekani, ili wasanii wetu nao wajisikie kuwa wana
eneo lao maalum", alisema Mlekwa.
Naye baba wa
Mwanasoka bora wa Tanzania Mzee Mbwana Samatta ameipongeza Serikali kwa
kumpatia mwanae eneo lenye ukubwa wa ekari tano ambapo mwanasoka huyo ameahidi
kujenga Kituo cha Michezo cha Vijana (Sports Academy) ili vijana ndani na nje
ya nchi waweze kuja na kupatiwa ujuzi na kupafanya mahali hapo kujulikana kote
ulimwenguni.
"Mbwana
Samatta ameniambia kuwa anataka kupafanya mahali hapa kuwa mahali pa Kimataifa
kwani anataka kuanzisha Kituo Maalum cha Wanasoka kuja kujifua hasa vijana wadogo
toka ndani na nje ya Tanzania", alisema mzee Samatta.
Katika hafla
hiyo, jumla ya wasanii 35 wamepatiwa vyeti vya umiliki wa maeneo yao pamoja na
ekari tano zimetolewa kwa ajili ya kumzawadia Mbwana Samatta kwa kuifanyia
Tanzania kung'ara katika soka ulimwenguni.




0 comments:
Post a Comment