Mohammed Dewji.
KAMPUNI tanzu ya MeTL Group, imeng’ara katika Tuzo za Rais za
Mzalishaji Bora wa Mwaka 2015 baada ya kutwaa tuzo tatu katika hafla
iliyofanyika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam. Tuzo hizo huandaliwa na
Shirikisho la Viwanda Nchini (CTI) na mwaka jana zilishirikisha zaidi ya
kampuni 350.
Katika hafla hiyo iliyohudhuriwa na Rais, John Magufuli, MeTL
inayoongozwa na Rais na Mkurugenzi Mtendaji, Mohammed `Mo’ Dewji ilitwaa
tuzo kupitia kampuni zake za Star Oils (T) Ltd inayohusika na bidhaa za
petroli, East Coast Foods & Fats inayozalisha bidhaa kadhaa ikiwa
ni pamoja na mafuta ya kula iliyokipa tuzo kiwanda hicho, na kiwanda cha
nguo cha 21st Century cha Morogoro.
Tuzo za mwaka huu zilihudhuriwa na watu takribani 300 kutoka sekta
binafsi na taasisi za serikali ikiwemo wafanyabiashara wakubwa pamoja na
wataalamu mbalimbali. MeTL Group yenye utajiri wa zaidi ya dola bilioni
1 (Sh trilioni 2.2) na inayoongoza kwa kutoa ajira upande wa sekta
binafsi ikiwa imeajiri watu 28,000 kwa Tanzania pekee, ilianzishwa
mwanzoni mwa miaka ya 1970 na Gulamabbas Dewji na tangu hapo imekua kwa
kasi kubwa kiasi cha sasa kuchangia asilimia 3.5 katika Pato la Taifa.
MeTL imejikita katika viwanda vya nguo, usagaji nafaka, utengenezaji
wa vinywaji baridi, usindikaji wa mafuta ya kula, usindikaji wa chai,
kilimo cha mazao mbalimbali yakiwemo mkonge, sekta ya nishati na
kadhalika.
Akizungumza baada ya tuzo hizo, Dewji alisema amehamasika kuona
kampuni yake inafanya vyema, huku akiahidi kuendelea kufanya kila
linalowezekana kutanua kampuni zake ili aweze kuongeza ajira na hivyo
kuisaidia serikali kupunguza tatizo la ajira kwa vijana na Watanzania
kwa ujumla.
Chanzo Gazeti La Habari Leo
0 comments:
Post a Comment