MKUU wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Mohammed Mpinga amesema
amepiga marufuku ya kuweka kioo cha giza sehemu ya mbele ya gari kwa
sababu trafiki wanapata shida kuwaona madereva wanaoendesha magari hayo
na pia huwa katika hatari ya kusababisha ajali barabarani.
Mpinga pia amesema kwamba agizo lake kuhusu kuwataka walioweka taa
zenye mwanga mkali kwenye magari yao, linahusu taa zote zikiwemo
zilizowekwa na wamiliki kama urembo pamoja na zile zilizowekwa kwenye
magari hayo viwandani zilizokotengenezwa.
Akizungumza na gazeti hili jana, Mpinga alitoa mfano wa dereva mmoja
aliyemgonga askari wa kike wa usalama barabarani aliyekuwa anaongoza
msafara kutokana na dereva huyo kuweka kioo cha giza cha mbele na hivyo
kutoweza kuona kikamilifu.
“Kama utakumbuka miaka michache iliyopita askari wetu wa kike
aligongwa pale Bamaga, tulifuatilia na kubaini kuwa dereva aliyemgonga
kuna uwezekano hakuwa anaona vizuri kutokana na kuweka kioo tinted (cha
giza) cha mbele,” alisema Mpinga.
Askari huyo aliyejulikana kwa jina la Elikiza alikuwa akiongoza
msafara wa Rais Jakaya Kikwete na baada ya msafara huo, aliruhusu magari
mengine yaendelee na safari, ndipo ghafla gari aina ya Landcruiser VX
lilipotoka upande wa pili na kumgonga wakati trafiki huyo anasimamisha
magari.
Alisema hata hivyo polisi haina takwimu za ajali ambazo zimesababishwa na kuwepo kwa magari yenye vioo vya giza,
“Takwimu hapa sina maana tumekuwa tunachukua tu takwimu kwa madereva
walevi, mwendo kasi na sababu zingine, lakini hiyo ya tinted kwa sasa
hatuna ila ninachosema ni hatari kwa usalama wa barabarani.”
Mpinga alisema pamoja na tukio hilo, askari wa usalama barabarani
wamekuwa wakipata usumbufu wanaposimamisha magari yenye vioo vya giza
mbele kwa kuwa hawamwoni anayeendesha gari.
“Wakati mwingine magari hayo yenye tinted kioo cha mbele wanaendesha
watoto ambao hawaruhusiwi kuendesha magari, na akisimamishwa dereva huyo
mtoto anaweza kubadilishana na mtu mwingine aliyembeba,” alisema
Mpinga.
Aliongeza kuwa askari anamwona anayeendesha gari pale tu dereva
anapofungua dirisha. Alisema kwa sheria za usalama barabarani dereva
anatakiwa aonekane hata kama amefunga vioo vya pembeni.
Alisema hata wale ambao wameweka vioo vya giza mbele wanapata wakati
mgumu kuona na ndio maana wakati mwingine wanalazimika kutoboa ili aone
kupitia vioo vya pembeni.
“Hii kwa usalama barabarani pia hairuhusiwi, unaweka tinted kali
kiasi hicho unaficha nini?’’ Alihoji Mpinga. Kuhusu magari yaliyowekwa
taa kali, Mpinga alisema baada ya kutoa agizo la kuwataka wamiliki
kuondoa taa hizo kwenye magari yao alipokea maoni ya kuomba taa
zilizowekwa kiwandani ziachwe kwa sababu hazikuwekwa na wamiliki.
“Lakini sisi tumeona kwamba taa hizo zenye mwanga mkali ambazo
zimewekwa kiurembo ziondolewe zote, hata zile ambazo zimewekwa huko
kiwandani,” alisema Mpinga na kufafanua kuwa atatoa taarifa zaidi leo
atakapozungumza na waandishi wa habari. James Yohana ni mmoja wa
madereva ambao wameweka vioo vya giza mbele ya gari lake alipoulizwa
sababu ya kufanya hivyo alisema, “Mimi niliweka kwa sababu tu sipendi
kuonekana kwa watu ninapoendesha gari, sina sababu nyingine,” alisema.
Alipoulizwa kama anafahamu kwamba gari zenye vioo giza zimepigwa
marufuku na polisi alisema kwamba anafahamu na tayari moja ya gari lake
ameshaondoa kioo cha giza na kwamba sasa atafanya hivyo katika gari lake
la pili.
Naye Abdul Muyanga mkazi wa Kipunguni Dar es Salaam alipoulizwa
sababu ya kuweka kioo cha giza sehemu ya mbele ya gari lake alijitetea
kwamba alifanya hivyo ili kujikinga na jua pamoja na kupendezesha gari
lake.
“Mimi nilifanya sio kwa nia mbaya, niliweka kujikinga na jua, lakini
pia ukiweka tinted mbele na kwenye vioo vya milangoni gari inapendeza,”
alisema Muyanga.
Aliongeza kuwa baada ya tangazo la kamanda Mpinga, anachofanya siku
hizi akifika kwenye taa za usalama barabarani anafungua madirisha yote
ili trafiki waweze kumwona anayeendesha gari.
Hivi karibuni Mpinga alitangaza kuzikamata gari zote ambazo zimeweka
vioo vya giza mbele. Pia aliagiza magari yote ambayo yamewekwa taa za
zenye mwanga mkali kuziondoa mara moja kwa kuwa zinawaumiza madereva
wengine na kusababisha ajali.
CHANZO GAZETI LA HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment