TUME ya Ushirikiano wa Pamoja ya Kudumu (JPCC) kati ya Tanzania na
Malawi, inatarajia kukutana nchini humo kwa ajili ya kujadili masuala
mbalimbali, ikiwemo la Watanzania nane kukamatwa nchini humo kwa tuhuma
za kuingia eneo la migodini bila kuwa na kibali.
Mbali na kujadili suala la Watanzania hao, lakini pia tume hiyo
itajidili mgogoro wa mpaka uliopo baina ya nchi hizo mbili katika Ziwa
Nyasa.
Mkutano huo unatarajiwa kuanza Februari 3 hadi 5 mwaka huu nchini Malawi.
Akizungumza Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Msemaji
wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mindi
Kasiga alisema tume hiyo ilikuwa haijakutana kwa muda mrefu, jambo
ambalo limesababisha watu kuwa na sintofahamu kati ya ushirikiano wa
nchi hizo mbili.
Kasiga alisema mkutano wa tume hiyo, mara ya mwisho ulifanyika mwaka
2003 jijini Dar es Salaam, hivyo kuwa kimya kwa muda mrefu kuna baadhi
ya watu walidhani kuwa ushirikiano wa nchi hizo mbili si mzuri.
“Kikao kama hiki kilikaa miaka mingi kidogo… kuna masuala
yaliyochelewa kutekelezwa kutokana na kukaa kwa kikao hiki, lakini kwa
sasa yatatekelezwa kupitia vikao hivyo,” alisema Kasiga.
Aliongeza kuwa kwa mara ya kwanza, vikao hivyo vitashirikisha
wafanyabiashara kutoka mikoa ya Njombe na Ruvuma, pia wavuvi kutoka
katika mikoa hiyo ambao wataeleza namna wanavyofanya shughuli zao kwa
kushirikiana na wenzao wa Malawi bila kuingilia.
Mindi alisema katika kikao hicho, ujumbe wa Tanzania utaongozwa na
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dk
Augustine Mahiga; na mbali na kujadili mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa na
Watanzania waliokamatwa, pia utajadili masuala mbalimbali katika sekta
za biashara, elimu, kilimo pamoja na sekta zingine.
Kasiga pia alikabidhi tuzo za Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa
Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania
(TRA) walizoshinda kutoka Umoja wa Afrika (AU). SSRA ambayo imekuwa wa
kwanza katika Tuzo za Ubunifu Katika Sekta za Umma Afrika (AAPSIA),
ilikabidhiwa kikombe pamoja na cheti cha ushindi.
Ushindi huo wameupata kupitia mradi wao wa Mradi wa Kanzidata ya Taifa ya Sekta ya Hifadhi ya Jamii.
Chanzo Gazeti la Habari leo
0 comments:
Post a Comment