Na Neema Mathias – MAELEZO
Chama
cha Walemavu Tanzania (CHAWATA) kimeiomba Serikali kuondoa kodi kwa
bajaji (pikipiki zenye magurudumu matatu) zinazotumiwa na watu wenye
ulemavu kama miguu na pia kubeba abiria ili kujipatia kipato.
Hayo
yamesemwa na Mwenyekiti wa CHAWATA John Mlabu mapema leo Jijini Dar es
Salaam, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu changamoto
na ajira kwa watu wenye ulemavu.
“Kupitia
fursa ya kuondolewa kodi kwa vifaa vya watu wenye ulemavu tunaiomba
Serikali izitambue bajaji kuwa ni moja ya nyenzo inayomsaidia mtu mwenye
ulemavu na hivyo ziondolewe kodi, na Serikali iziagize kwa wingi na
kuzikabidhi kwa watu wenye ulemavu kwa mkopo kupitia Umoja wa Waendesha
Bajaji Dar es Salaam (UWAWABADA),” amesema Mlabu.
Ameendelea
kwa kusema, kupitia UWAWABADA bajaji hizo zitatawanywa kote nchini kwa
utaratibu walionao ili ziwainue kiuchumi na kuboresha maisha yao na
familia zao.
Aidha
Mlabu amesema, CHAWATA kinamuomba Rais Dkt. John Pombe Magufuli na
Serikali yake kuangalia kundi hilo kupitia mafanikio ya watu wenye
ulemavu Jijini, Dar es Salaam na kurasimisha shughuli ya uendeshaji wa
bajaji kuwa ya watu wenye ulemavu pekee na wengine wasio na ulemavu
waendeshe pikipiki za kawaida (Bodaboda).
“Kuendesha
Bajaji ni ajira pekee ambayo haina usumbufu kwetu na imeyagusa makundi
yote ya wanawake na wanaume tena rika zote, maana kwenye ujenzi wa
viwanda na makampuni sisi hatuajiriwi, licha ya uwepo wa sheria Na. 9 ya
2010 ya ajira kwa walemavu inayotaka kila mahali pa kazi 3% ya
watumishi wake wawe watu wenye ulemavu,” amefafanua Mlabu.
Vile
vile amesema, uwepo wa chombo hicho cha magurudumu matatu kimewasaidia
sana walemavu kujipatia kipato na kuwaondoa katika maisha ya kuombaomba
kama ilivyokuwa hapo awali, aidha amesema kuwa wanaichangia Serikali
katika kukuza uchumi wa nchi kupita kodi mbalimbali za Serikali pale
wanaponunua mafuta ama vipuli vya bajaji zao.
CHAWATA
kimeipongeza Serikali ya Awamu ya Tano na Rais Dkt. Magufuli kwa kujali
watu wa tabaka la chini na maskini katika Taifa hili, ambapo
wameshuhudia mara nyingi katika ziara zake akiwatetea wafanyabiashara
wadogo (Machinga), Wakulima na Wafugaji, hivyo wanamuona Rais Magufuli
kuwa ni Rais wa wanyonge.
0 comments:
Post a Comment