Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Na. Mwandishi Wetu
Waziri
wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe ameunda
Kamati ya wajumbe kumi itakayoongozwa na Mkurugenzi wa Idara ya Habari
(MAELEZO) Dkt. Hassan Abbasi, kuchunguza ufanisi katika mkataba baina ya
Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) na Kampuni ya Star Times.
Taarifa
iliyotolewa na Kitengo cha Mawasiliano cha Wizara ya Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo inaeleza kuwa mbali na Dkt. Abbasi, wajumbe
wengine wanaunda Kamati hiyo kutoka upande wa Tanzania ni Bw. Kyando
Evod kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Frederick
Ntobi na Injinia James Kisaka wote kutoka Mamlaka ya Mawasiliano
Tanzania (TCRA) na Bw. Mbwilo Kitujime kutoka TBC.
Aidha, taarifa
hiyo imeeleza kuwa majina ya wajumbe wengine watano walioteuliwa kutoka
upande wa China yatawasilishwa ili kukamilisha idadi ya wajumbe kumi wa
Kamati hiyo.
“Kamati imepewa hadidu za rejea takribani nane na
inatakiwa kufanya kazi kwa muda wa siku saba kukamilisha kazi hiyo”,
inaeleza taarifa hiyo.
Kamati hiyo imeundwa kufuatia kutopatikana
kwa faida kwa kipindi cha miaka saba sasa katika mkataba baina ya TBC
na Kampuni ya Star Times.
Kabla ya kuunda Kamati hiyo, jana
Waziri Mwakyembe alikutana na Mwenyekiti wa Kampuni ya Star Times kutoka
China, Xinxin Pang kujadiliana kwa kina juu ya mkataba huo ambapo
katika majadiliano hayo walikuwepo wafanyakazi wa Wizara hiyo akiwemo
Katibu Mkuu, Profesa Elisante Ole Gabriel na Mkurugenzi wa Idara ya
Habari (MAELEZO) Dkt. Abbasi.
Sakata la mkataba baina ya TBC na
Star Times lilichukua sura mpya baada ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli
kutembelea ofisi za TBC mwezi Mei mwaka huu na kuonesha kukerwa na
kutopatikana kwa faida katika
mkataba huo kwa kipindi cha miaka saba na kuagiza kuchukuliwa kwa hatua stahiki.
0 comments:
Post a Comment