Imeandikwa na Mwandishi Maalumu
WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amewahakikishia uwekezaji wenye tija
wawekezaji watakaokuja nchini kwa kuwa Tanzania ni nchi yenye amani,
utulivu wa kisiasa na uchumi wenye kukua kwa kasi.
Aliyasema hayo jijini Dar es Salam jana alipomuwakilisha Rais John
Magufuli katika maadhimisho ya miaka 60 tangu Mtukufu Aga Khan
alipochaguliwa kuwa Imamu Mkuu wa madhehebu ya Shia Ismailia duniani.
Waziri Mkuu alisema Serikali inatambua na kuthamini shughuli mbalimbali
zinazofanywa na mtandao wa taasisi za Aga Khan zilizopo hapa nchini,
hivyo Serikali itaendelea kushirikiana nao.
Aliupongeza mtandao wa taasisi za Aga Khan kwa kumuunga mkono Dk
Magufuli katika kutoa kipaumbele cha kuwapa fursa watu wenye kipato cha
chini kushiriki katika uzalishaji ili waweze kujikwamua kiuchumi.
“Nawahakikishia kwamba uwekezaji wenu hapa nchini utakuwa na baraka kwa
sababu nchi imetulia kisiasa na uchumi wake unakua kwa kasi.
Nawaomba muendelee kuwaalika wanajumuia wa madhehebu ya Shia Ismailia
popote walipo duniani waje kuwekeza nchini fursa bado zipo.” Kwa upande
wake Rais wa Jumuiya ya Madhehebu ya Shia Ismailia Tanzania, Amin
Lakhani ameishukuru Serikali kwa ushirikiano inaowapa na kwamba ameahidi
kuendelea kushirikiana nayo katika kuboresha sekta mbalimbali nchini.
Alisema mtandao wa maendeleo wa Aga Khan unatoa huduma mbalimbali
zikiwemo za afya, elimu, kilimo na kunaendesha miradi katika mabara ya
Afrika na Asia kwa kuwapa fursa watu wenye kipato cha chini kushiriki
katika uzalishaji ili kujikwamua kiuchumi. Awali, Mkuu wa wilaya ya
Ilala, Sophia Mjema aliipongeza taasisi hiyo kwa mpango wake wa upanuzi
wa hospitali na kuongeza vituo 35 vya afya kutoka 15 walivyonavyo.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment