Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » MANJI ASHINDWA KUHUDHURIA KORTINI

MANJI ASHINDWA KUHUDHURIA KORTINI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Imeandikwa na Fransisca Emmanuel


Aliyekuwa Mwenyekiti wa Yanga, Yusuph Manji

WAKILI wa Serikali Mwandamizi, Nassoro Katuga ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kuwa amepata taarifa kutoka kwa daktari wa Magereza kwamba mfanyabiashara Yusuf Manji (41), amepelekwa katika Hospitali ya Gereza la Keko kwa kuwa hali yake sio nzuri.
Katuga alidai hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutajwa jana. Alidai Manji ameshindwa kufika mahakamani hapo kwa kuwa anaumwa na amepelekwa hospitalini hapo kwa ajili ya   matibabu na kwamba washitakiwa wengine wapo.
Mbali na Manji, washitakiwa wengine ni Meneja Rasilimaliwatu wa Kampuni ya Quality Group Ltd, Deogratius Kisinda (28), Mtunza stoo, Abdallah Sangey (46) na Thobias Fwere (43), mkazi wa Chanika wanakabiliwa na mashitaka ya uhujumu uchumi.
Aidha, Katuga alidai upelelezi wa shauri hilo haujakamilika, lakini upo katika hatua za mwisho. Wakili wa washitakiwa, Hudson Ndusyepo alidai hawana shaka na lililoongelewa na upande wa mashitaka lakini wa naomba upelelezi ukamilike.
Hakimu Shaidi aliahirisha kesi hiyo hadi Agosti 4 mwaka huu kwa ajili ya kutajwa. Inadaiwa Juni 30, mwaka huu maeneo ya Chang’ombe A wilayani Temeke Dar es Salaam, washitakiwa wote kwa pamoja, walikutwa na askari polisi wakiwa na mabalo 35 ya vitambaa vinavyotumika kutengenezea sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) vyenye thamani ya Sh milioni 192.5.
Pia inadaiwa Julai mosi mwaka huu, maeneo ya Chang’ombe A, wilayani Temeke, Dar es Salaam, washitakiwa wote walikutwa na askari polisi wakiwa na mabalo nane ya vitambaa vinavyotumika kutengenezea sare za JWTZ vyenye thamani ya Sh milioni 44.
Katika mashitaka ya tatu, inadaiwa Juni 30, mwaka huu maeneo ya Chang’ombe A, washitakiwa walikutwa wakiwa na mhuri wa JWTZ ambao uliandikwa ‘Mkuu wa Kikosi 121 Kikosi cha JWTZ’ bila kuwa na uhalali kitendo kinachohatarisha usalama wa nchi.
Pia inadaiwa, terehe hiyohiyo maeneo ya Chang’ombe washitakiwa walikutwa na mhuri uliokuwa umeandikwa ‘Kamanda Kikosi 834 KJ Makutupora Dodoma’ bila kuwa na uhalali kitendo kinachohatarisha usalama.
Ilidaiwa Juni 30, mwaka huu, maeneo hayo, washitakiwa kwa pamoja walikutwa na mhuri ulioandikwa ‘Commanding Officer 835 KJ, Mgambo P.o. Box 224 Korogwe’ isivyo halali. Katika mashitaka ya sita, inadaiwa Julai Mosi mwaka huu, maeneo hayo ya Chang’ombe, washitakiwa walikutwa na gari lenye namba za usajili SU 383 mali waliyojipatia isivyo halali.
Aidha, wanadaiwa kuwa Julai Mosi mwaka huu, maeneo ya Chang’ombe A wilayani Temeke, Dar es Salaam, washitakiwa wote walikutwa na gari lenye namba za usajili SM 8573 pasipo uhalali.
Washitakiwa hawakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa sheria ya uhujumu uchumi na ya usalama wa Taifa haijaipa mamlaka mahakama kusikiliza kesi hiyo. Upande wa mashitaka ulidai wamepata hati ya kupinga dhamana kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kuomba washitakiwa wasiruhusiwe kupewa dhamana kwa sababu wakiachiwa watahatarisha usalama na maslahi ya nchi. Pia alidai kwenye mashitaka ya kwanza na ya pili, Mahakama ya Kisutu haina mamlaka ya kushughulikia masuala ya dhamana.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa