Imeandikwa na Mwandishi Wetu
SERIKALI imetoa ufafanuzi kuhusu matamshi iliyoyaita ya kichochezi na
yenye kuudhi, yaliyotolewa na Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu
kuwa inabana demokrasia na kusema kuwa matamshi hayo ni propaganda
zilizoendeshwa kwa minajili ya kisiasa.
Aidha, imemshauri Lissu ambaye pia ni Wakili wa Mahakama Kuu, kufanya
kazi yake kwa weledi na kusimamia maadili na si kuupotosha umma kwa
sababu zake za kisiasa. Katika taarifa aliyoitoa kwa umma jana, Msemaji
Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO),
Dk Hassan Abbas, alisema matamshi ya Lissu yalinukuliwa na vyombo
mbalimbali vya habari juzi, pia yalikejeli Mahakama.
Kwa mujibu wa Dk Abbas, serikali itaendelea kuenzi na kuilinda
misingi ya demokrasia, uhuru wa watu na kuwapa fursa wananchi kushiriki
katika uchumi wa nchi hasa wakati huu wa mageuzi makubwa ya kiutendaji
chini ya Rais John Magufuli.
Hata hivyo, alisema “Lakini serikali haitavumilia mtu yeyote au
kikundi chochote kitakachojaribu kutumia uhuru wowote vibaya ili tu
kukwaza azma hiyo ya Taifa”. Alimuasa Lissu pamoja na wananchi kwa
ujumla, kujiepusha na propaganda, kejeli na uzushi usio na msingi dhidi
ya serikali au taasisi zake.
Zaidi, alitoa mwito kwa Lissu na wananchi kwa ujumla kutafuta haki
kupitia mkondo wa sheria, badala ya kuvunja sheria, ikiwa wataona kuna
haki zimekiukwa. Alifafanua kwa nini alichotamka Lissu ni propaganda za
kisiasa na kusema alichanganya kati ya haki katika demokrasia, ambazo
hata yeye amezitumia kuzungumza na wanahabari bila tashtiti kwa upande
mmoja na misingi ya wajibu kwa upande mwingine ambayo kila mmoja, iwe
Tanzania au kwingineko duniani, anayo na pale anapokiuka hatua
huchukuliwa.
Alisema tofauti na upotoshaji wa Lissu, Tanzania ikiwa nchi kiongozi
Afrika na duniani katika kuenzi demokrasia na kupigania haki, si tu
inaendelea kuenzi misingi hiyo, bali pia imechukua hatua za wazi
kuhakikisha kuwa misingi hiyo inalindwa na pale mtu na hata taasisi
zinapokiuka, mkondo wa sheria huchukua nafasi yake.
“Ikiwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa (UN), Tanzania imeridhia
Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa wa mwaka 1966 na
huwasilisha taarifa zake za utekelezaji wa demokrasia na haki za
binadamu katika Kamisheni ya UN ya Haki za Binadamu,” alisema Dk Abbas.
Pia, alieleza kuwa Kikanda, Tanzania ikiwa mwanachama kiongozi wa
Umoja wa Afrika (AU) imeridhia Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na
Watu na ni miongoni mwa nchi za kwanza Afrika kukubali kushtakiwa na
wananchi wake kwa kuridhia itifaki ya Mahakama ya Afrika ya Haki za
Binadamu na pia kukubali kufanyiwa ukaguzi katika utawala bora kupitia
Mpango wa Afrika Kujitathmini Kiutawala Bora (APRM).
Kitaifa, pamoja na kuruhusu taasisi anuai za umma na binafsi, Dk
Abbas alisema Serikali ya Tanzania ni miongoni mwa mataifa machache
Afrika yaliyotunga sheria ya ndani ya nchi inayowapa wananchi wake haki
ya kuishitaki serikali au watu wengine wanapoona wamevunjiwa haki zao za
kidemokrasia au kibinadam
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment