Imeandikwa na Mwandishi Wetu
SERIKALI imevunja Bodi ya Baraza la Taifa la Hifadhi ya Usimamizi wa
Mazingira (NEMC), sambamba na kufanya mabadiliko ya uongozi huku
watumishi wanne wakisimamishwa kazi kupisha uchunguzi wa tuhuma
zinazowakabili.
Akizungumza jana na waandishi wa habari, Waziri wa Nchi, Ofisi ya
Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba alisema hatua
hiyo imetokana na kukithiri kwa malalamiko ya wananchi na wawekezaji wa
ndani na nje ya nchi.
“Tunapoelekea kuwa nchi ya uchumi wa viwanda, usimamizi wa mazingira
lazima uwe imara na urahisishe na kuharakisha utekelezaji wa ujenzi wa
viwanda, miradi mbalimbali na uwekezaji katika sekta zote ili kwenda kwa
kasi na weledi unaotakiwa,” alieleza January.Aliongeza: “Utendaji wa
NEMC umekuwa ukilegalega sana na umekuwa hauridhishi jambo ambalo
limeibua malalamiko mengi kwa wawekezaji wa ndani na nje.”
“Tumejitahidi kurekebisha hali hii na kumejitokeza nafuu, lakini bado
hali haijafikia pale nilipotarajia. Nimefuatilia kwa karibu na kugundua
kuwa matatizo mengi yanasababishwa hasa na usimamizi usio imara wa bodi
na pia watendaji wakuu wa NEMC.
Nimeamua kutengua uteuzi wa wajumbe wote saba wa Bodi ya NEMC ili
baadaye niteue wajumbe wapya ambao wataenda na kasi na ari tunayoihitaji
sasa katika kuelekea uchumi wa viwanda.” Alisema Mwenyekiti wa Bodi
ambaye mamlaka yake ya uteuzi ni ya Rais, ataendelea kuwepo hadi hapo
atakapoteuliwa mwingine. Alisema amemteua Dk Elikana Kalumanga, kuwa
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NEMC hadi hapo rais atakapofanya uteuzi kwa
nafasi hiyo. Kalumunga ni Mhadhiri katika Taasisi ya Usimamizi na
Tathmini ya Rasilimali Asili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).
Alisema ili kuboresha utendaji wa NEMC, amefanya mabadiliko ya baadhi
ya wakurugenzi na wakuu wa kanda, kwa Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa
NEMC, Charles Wangwe kumrejesha Wizara ya Fedha na Mipango
atakapopangiwa kazi kulingana na mahitaji ya serikali.
Nafasi hiyo itakaimiwa na Adam Minja kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.
Aliwataja wakuu wa kanda waliobadilishwa ni Jafari Chimgege aliyekuwa
Kanda ya Mashariki anakwenda Kanda ya Kati- Dodoma, Goodlove Mwamsojo
aliyekuwa Mkuu wa Kanda ya Nyanda za Juu –Mbeya atakuwa Mkuu wa Kanda ya
Mashariki- Dar es Salaam.
Pia Dk Ruth Rugwisha aliyekuwa Mkuu wa Kurugenzi ya Ufuatiliaji na
Uzingatiaji wa Sheria, sasa atakuwa Mkuu wa Kanda ya Ziwa-Mwanza, Dk
Vedastus Makota aliyekuwa Mkurugenzi wa Mawasiliano na Elimu kwa Umma
atakuwa Mkuu wa Kanda ya Kusini- Mtwara na Joseph Kombe aliyekuwa Mkuu
wa Kurugenzi ya Utafiti na Mipango wa NEMC anakwenda kuwa Mkuu wa Kanda
ya Kaskazini- Arusha.
Mabadiliko hapo pia yamemgusa Dk Menard Jangu aliyekuwa Arusha ambaye
anapanda na anarudishwa Makao Makuu ya NEMC kuwa Kaimu Mkuu wa
Kurugenzi ya Utafiti na Mipango huku Jamal Baruti aliyekuwa Mkuu wa
Kanda ya Ziwa anarudi Makao Makuu na Lewis Nzari aliyekuwa Mkuu wa Kanda
ya Kusini -Mtwara, sasa anakuwa Mkuu wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini-
Mbeya. Pia Risper Koyi wa Ofisi ya Makamu wa Rais ameteuliwa kuwa Kaimu
Mkuu wa Kitengo cha Sheria NEMC kuchukua nafasi ya Jandwa anayehamishiwa
Kanda ya Kati-Dodoma.
Pia Dk Yohana Mtoni ambaye ni Ofisa Mazingira Mkuu NEMC anakuwa Kaimu
Mkuu wa Idara ya Ufuatiliaji na Uzingatiaji wa Sheria kumbadili
Rugwisha ambaye anakwenda Kanda ya Ziwa- Mwanza, na Carlos Mbuta
aliyekuwa Ofisa Mawasiliano Mkuu wa NEMC ameteuliwa kuwa Kaimu
Mkurugenzi wa Mawasiliano na Elimu kwa Umma wa NEMC. Aidha, January
alisema wamewasimamisha kazi watumishi watumishi wanne ili kupisha
uchunguzi kutokana na tuhuma za utendaji wao; ambao ni mwanasheria
Manchare Heche, Deus Katwale, Andrew Kalua na Benjamin Dotto.
Alifafanua kuwa malalamiko yaliyokithiri NEMC ni ucheleweshaji na
urasimu usiokuwa wa lazima katika mchakato wa Tathmini ya Athari kwa
Mazingira (EIA), tuhuma za rushwa katika mchakato wa ukaguzi na
utengeneza vyeti ambavyo havijafuata mchakato.
Alisema pia kumekuwapo na malalamiko ya kutokuwa na lugha nzuri kwa
wateja na kuwatisha ili watoe chochote, kutumia kampuni binafsi ya
watumishi wa NEMC kufanya kazi za ukaguzi kwa kisingizio cha kutokuwa na
watumishi wa kutosha na kuwaelekeza wawekezaji kufanya kazi na kampuni
inayomilikiwa au yenye ubia na watumishi hao.
Katika hatua nyingine, January ameagiza ruksa ya ujenzi itolewe ndani
ya siku tatu za kazi kwa miradi yote inayohusu ujenzi wa viwanda, baada
ya mwekezaji kuwasilisha taarifa hitaji la ujenzi wa kiwanda kwa NEMC.
Alisema kuanzia sasa miradi itakayopelekwa NEMC kuombewa cheti cha EIA
ni ile ambayo tayari imefanyiwa kazi na washauri elekezi. “Hapatakuwepo
na haja ya kusajili mradi NEMC kwanza.
NEMC itaweka maofisa katika Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) na
maeneo mengine muhimu ili kuhakikisha suala la kuwa na cheti cha
mazingira linakuwa sehemu ya hatua za awali pale ambapo mwekezaji au
mwenye mradi anapoanza kuomba vibali ingine.
Pia ameagiza NEMC ndani ya wiki hii kufuta watu binafsi na kampuni
zote za ushauri wa EIA ambayo hayana sifa au yameshindwa kutekeleza kazi
zao vizuri, na ameagiza iweke bei elekezi na ukomo kwa washauri kwa
kila aina ya miradi inayotakiwa kufanyiwa EIA.
CHANZO HABARI LEO.
0 comments:
Post a Comment