Imeandikwa na Mwandishi Wetu
SERIKALI imeahidi kuzidisha mapambano dhidi ya rushwa na ukiritimba
kwenye mamlaka zinazohusiana na uwekezaji nchini ili kuwavutia
wawekezaji zaidi hususani kutokea nchini China, hatua iliyotajwa kuwa
itaongeza kasi zaidi kwenye uwekezaji kwenye sekta ya viwanda nchini.
Akizungumza wakati akifungua Mkutano wa Sita wa Mwaka wa Taasisi ya
Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF) uliofanyika jijini Dar es Salaam
jana, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Phillip Mpango (pichani)
aliyemwakilisha Makamu wa Rais, Samia Suluhu, alisema ni vigumu kwa
serikali kufanikisha azma yake ya kufikia uchumi wa viwanda ikiwa
vitendo vya rushwa na ukiritimba vitakithiri kwenye mamlaka zinazohusika
na uwekezaji nchini.
“Nia hasa ni kunufaika na fursa za kiuwekezaji kutoka mataifa makubwa
ikiwemo China ambao kimsingi wamekuwa washirika wetu kwa miaka mingi.
Hata hivyo, tunaamini kuwa kama taifa, bado tunahitaji kunufaika zaidi
na uwekezaji kutoka China na ndiyo maana tunaweka msisitizo zaidi katika
kukabiliana na kila aina ya changamoto inayoweza kukwamisha unufaikaji
huo ikiwemo rushwa na ukiritimba kwenye mamlaka zetu za kiuwekezaji,”
alieleza Dk Mpango.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment