Imeandikwa na Waandishi Wetu
WAZAZI wa wanafunzi Mugisha Lukambu na Atuganile Jimmy ambao ni
miongoni mwa wanafunzi 10 wa mchepuo wa sayansi wamebainisha kuwa
walilazimika kuwajengea misingi mizuri watoto wao tangu wakiwa na umri
mdogo baada ya kubaini kipaji chao.
Mugisha (Feza Boys) na Atuganile (Feza Girls) ni miongoni mwa
wanafunzi 10 bora wa masomo ya sayansi katika matokeo ya Kidato cha Sita
ambao katika matokeo ya kidato cha nne ya mwaka 2014 walikuwa miongoni
mwa wanafunzi 10 bora kitaifa.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Musoma, baba mzazi wa Mugisha,
Reynold Lukambuzi alisema mtoto wao alionesha kipaji akiwa mdogo jambo
ambalo liliwasukuma kumpeleka shule mapema.
Mugisha na Atuganile ni miongoni mwa nwafunzi 10 bora wa masomo ya
sayansi katika matokeo ya Kidato cha Sita ambao mwaka 2014 katika
matokeo ya kidato cha nne walikuwa miongoni mwa wanafunzi 10 bora
kitaifa.
Mugisha aliyekuwa akisoma Shule ya Sekondari ya Bendel Memorial
alishika nafasi ya tano, wakati Atuganile aliyemaliza Shule ya Sekondari
ya Canossa alishika nafasi ya nane. Akizungumza na gazeti hili kutoka
Musoma, Lukambuzi ambaye ni mwalimu mstaafu alisema, “Mugisha alikuwa na
kipaji, alikuwa na uwezo wa kupambanua mambo makubwa tofauti na umri
wake, jambo ambalo lilitusukuma kumpeleka shule mapema akiwa na umri wa
miaka mitatu.”
Alisema ili kuendeleza kipaji chake, yeye na mzazi mwenzake Yustina
Lukambuzi, waliamua kumpeleka kwenye shule za kulipia wakiamini ndio
shule ambazo zingeweza kumjenga na kuendeleza kipaji chake. Alisema
alipata elimu ya msingi katika shule ya Emmanuel iliyopo Musoma mjini
ambako alifanya vizuri na baadaye kumpeleka shule ya kulipia ya Bendel
Memorial iliyoko Moshi mkoani Kilimanjaro ambako alimaliza elimu ya
kidato cha nne.
Mugisha ambaye katika matokeo ya kidato cha sita akiwa amepanda
nafasi moja hadi kuwa nafasi ya nne ukilinganisha na yale ya kidato cha
nne, kwa sasa yuko kwenye mafunzo ya hiyari ya Jeshi la Kujenga Taifa
(JKT) Songea.
Alisema kutokana na kufanya vizuri akiwa kidato cha nne, Mugisha
alipata fursa ya kusomeshwa miaka miwili bure katika Shule ya Sekondari
ya Feza Boys jijini Dar es Salaam akichukua masomo ya tahasusi ya PCB
(Fizikia, Kemia na Baiolojia).
“Kwa kweli tumepokea matokeo kwa furaha kubwa, kipaji chake ndicho
kilichotufanye tumepeleke shule za private, na ndicho kilichofanya
asomeshwe bure kwa miaka miwili na Shule ya Sekondari ya Feza,” alisema.
Naye baba mzazi wa Atuganile aliyechukua masomo ya tahasusi ya PCM
(Fizikia, Kemia na Hisabati), Cairo Jimmy alisema “Tumefurahi kwa
mwanetu kwanza kushirikilia namba ile aliyoipata kwenye matokeo ya
kidato cha nne. Ni binti ambaye anapenda kusoma na mara nyingi amekuwa
akinisimbua kwa kuhitaji vitabu mbalimbali vya kujisomea.”
Aliongeza: “Tulichofanya sisi kama wazazi ni kumuwekea msingi mzuri
wa somo la hisabati tangu akiwa darasa la kwanza, na tushukuru naye
aliitikia mwito kwa kusoma vizuri na kupenda sana Hisabati.
“Mimi nilikuwa mzuri kwenye hesabu kwenye shule ya msigi na sekondari
kidogo, lakini Atuganile alikuwa ni wa pekee kwani hata mimi wakati
mwingine alinizidi jambo ambalo lilinifanya nimtafute raifiki yangu
(Twahili Mshana),” alisema.
Alisema Atuganile aliyemaliza elimu ya msingi katika Shule ya Msingi
Mwangaza iliyopo Gongo la Mboto, Ilala alifaulu vizuri na kupangiwa
shule ya wanafunzi wenye vipaji ya Tabora.
“Alipangiwa Tabora, lakini tuliamua tujifunge mikanda na kujibana ili
akasome Canossa ambako aliongoza katika kipindi chate cha masomo yake,”
alisema. Alisema baada ya matokeo ya kidato cha nne, alifuatwa na
uongozi wa Feza ambao walitaka akasome katika shule hiyo.
“Kwa sababu Atuganile aliongoza Mkoa wa Dar es Salaam walipokuwa
wakipewa zawadi, Feza walitufuata, lakini si unajua shule hizo ada yao
ni kubwa, lakini wao walitaka akasome na kutupunguzia ada kutoka
shilingi milioni tisa hadi kulipa shilingi milioni 1.5 kwa mwaka,”
alieleza.
Jimmy ambaye yeye ni mhasibu, alisema awali mtoto wao walimshauri
akasomee udaktari kutokana na kushika nafasi ya tatu kwenye somo la
baolojia, lakini aligeuka na kukataa kusoma PCB kwa madai hakuna hesabu.
“Awali tulikubaliana akasome udaktari, lakini alivyoenda Feza alisema
atasoma PCM kwa sababu PCB haikuwa na hesabu, na yeye alitaka kuendelea
na hesabu zake, lakini sasa amebadili mtazamo na kutaka kujihusisha na
masuala ya ndege,” alifafanua mzazi huyo.
Kwa upande wake, uongozi wa Shule ya Sekondari ya Mwenyeheri Anuarite
umeeleza sababu zilizowaweka kwenye kundi la shule 10 zilizofanya
vibaya katika matokeo ya mtihani wa Taifa wa kidato cha sita mwaka huu
ikiwemo kuwa darasa la kwanza kuhitimu kidato cha sita na nidhamu hafifu
kwa baadhi ya wanafunzi.
Aidha, umesema pia kuwa pamoja na kuwa nafasi ya nne katika kundi
hilo jambo lililowashtua na wao baada ya kusikia matokeo hayo, lakini
kiuhalisia wahitimu katika shule hiyo walikuwa 30 na kati yao, wanafunzi
sita ndio waliopata sifuri na watatu daraja la nne.
Waliopata daraja la tatu ni 15, la pili ni watano na daraja la kwanza
ni mmoja. Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake jana, Mkuu wa Shule
hiyo inayomilikiwa na Parokia ya Mtakatifu Gaudence, Makoka, Jimbo Kuu
la Dar es Salaam, Carlos Mgumba alisema wamejifunza kutokana na makosa
kadhaa yaliyojitokeza ikiwemo ndio wahitimu wa kwanza wa kidato cha sita
kwa shule hiyo.
“Kuna mambo kadhaa tumejifunza kutokana na uchanga wetu wa darasa
hili la kwanza kuhitimu kidato cha sita kwetu mwaka huu. Wengi wa
wanafunzi wetu hapa ni wa mchepuo wa sanaa na wote wamefaulu vizuri,”
alisema Mgumba.
Alisema wanafunzi wote waliopata sifuri ni wa mchepuo wa sayansi na
wengi wao ni waliogoma waliposhauriwa kubadilisha mchepuo tangu wakiwa
kidato cha tano baada ya kuonekana ufaulu wao si mzuri katika eneo la
sayansi.
Mwalimu Mgumba alisema walianza wakiwa na wanafunzi 13, lakini
wengine walihamia na kuongeza changamoto ya kuwa na uelewa mmoja tofauti
na walioanza na walimu tangu awali.
Akifafanua zaidi kuhusu sababu za kufanya vibaya, alisema kuna baadhi
ya wanafunzi waliibuka na kuwa na tabia zisizoridhisha na walipofikiria
kuwapumzisha nyumba (ni shule ya bweni) kama walivyofanya shule
nyingine za kanisa, waliona sababu ni darasa la kwanza la elimu ya juu
ya sekondari (A Level), watawavunja moyo na kuwaacha lakini wengi ndio
waliofeli.
“Hakuna mwanafunzi aliyesikiliza mwalimu vizuri darasa, amefeli, kuna
walioshauriwa kubadili mchepuo baada ya kuonekana masomo waliochagua,
hawawezi na waliokubali, wamepata daraja la pili na la tatu,” alisema
Mgumba.
Kuhusu umahiri wa walimu, Mgumba alisema ana ujasiri wa kusimama
popote kuelezea umahiri mkubwa wa walimu waliopo katika shule hiyo kwa
uzoefu wa ufundishaji, elimu zao, shule walizofundisha ambazo baadhi ni
za kanisa zilizopo katika 10 bora na nidhamu kubwa ya kazi pamoja na
idadi yao kukidhi mahitaji.
Alisema kwa wastani kwa kidato cha tano na cha sita, kila somo
linafundishwa na walimu wawili na maabara ina vifaa vyote kwa ajili ya
masomo ya sayansi. Hata hivyo, alisema ili kuondoa sifuri katika shule
yao, alikutana na wanafunzi wa kidato cha sita mwaka huu na walimu
kuwatia moyo ili wajitambue kuwa wanaweza kufanya vizuri zaidi na
matokeo si ya kusitisha hivyo yasiwakatishe tamaa.
Alisema kama shule, wamejizatiti kuongeza mitihani ya majaribio kila
wiki kwa wanafunzi wa kidato cha sita, wameanzisha kitengo cha ushauri
wa masuala ya elimu na binafsi kwa wanafunzi ili wawe huru kujieleza
wanapoona kuna tatizo na ushauri hufanywa na watu wa nje ili wawe huru
kujieleza.
Wakizungumzia matokeo na namna walivyojipanga kufanya vizuri katika
mitihani yao, Kaka Mkuu wa Shule, Teophily Mbiro anayesoma PCB, alisema
walipokea kwa huzuni matokeo ya wenzao na wamekutana na mkuu wa shule na
walimu na kukubaliana kutorudia makosa ya wenzao.
Shule zilizo katika kundi la 10 zilizofanya vibaya katika matokeo ya
kidato cha sita yaliyotangazwa na Baraza la Mitihani la Taifa (Necta)
Jumamosi ambayo wasichana waliongoza kwa ufaulu na idadi ya wanafunzi
katika shule hizo kwenye mabano ni Kiembesamaki, Unguja (120), Hagafilo,
Njombe (53), Chasasa, Pemba (76), na Mwenyeheri Anuarite, Dar es Salaam
(30).
Nyingine ni Ben Bella, Unguja (108), Meta, Mbeya (300), Mlima Mbeya,
Mbeya (59), Njombe, Njombe (455), Al-Ihsan Girls, Unguja (41) na St
Vicent, Tabora (31). Imeandikwa na Gloria Tesha na Anastazia AnyimCHANZO HABARI LEO.
0 comments:
Post a Comment