Imeandikwa na Alfred Lasteck
IDARA ya Uhamiaji nchini imewataka wananchi kutambua kuwa paspoti
siyo kitambulisho ndani ya nchi na kwamba kisitumike kwa matumizi hayo
kwa sababu siyo utaratibu uliopangwa kisheria ndani ya mipaka ya nchi.
Pia amesema kuwa ikibainika kuwa mtu amepoteza paspoti hiyo kizembe
hatopewa nyingine. Hayo yalisemwa jana jijini Dar es Salaam na Kamishna
wa Uhamiaji- Pasi na Uraia, Gerald Kihinga wakati alipofanya mahojiano
maalumu na gazeti hili, na kuwaomba wananchi kutambua kuwa paspoti
zinazotolewa zinapaswa kutunzwa na kutumika kwa lengo lililokusudiwa la
kusafiria nje ya nchi.
Kihinga alisema kumekuwa na maombi ya kutengenezewa paspoti baada ya
kupotezwa, lakini wengi wamekuwa wakitoa sababu ambazo zinatilia shaka
umakini wa mtu kwenye utunzaji wake. “Naomba mfahamu kuwa paspoti pia
zinazotolewa siyo vitambulisho ndani ya nchi hivyo visitumike kama
vitambulisho na tena si vizuri kutembea nayo kila mahali kama huna
safari ya nje ya nchi.
Paspoti au hati ya kusafiria zinatumika kama kitambulisho pale
unapokuwa nje ya nchi, lakini matumizi yake rasmi ni ya kukusaidia
kuingia na kutoka nchini,” alisema. Alisisitiza kuwa kitambulisho rasmi
cha Mtanzania anachotakiwa kutembea nacho ni kile kinachotolewa na
Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA). Aidha, kamishna huyo pia
ametaka wananchi raia wa Tanzania kutambua kuwa wanaweza kupata paspoti
wakiwa popote Tanzania na kwa muda mfupi.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment