Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), Deusdedit
Kakoko ameiomba serikali kuipatia mamlaka hiyo vitendeakazi muhimu ili
kukabiliana na vitendo vya uharamia wa bomba la mafuta katika Bahari ya
Hindi.
Kakoko ametoa maombi hayo kwa Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip
Mpango aliyetembelea bandari hiyo upande wa mafuta na kuelezwa kuhusu
tukio lililotokea juzi baada ya TPA kukamata boti moja iliyokuwa
ikitumiwa na wahalifu kuiba mafuta kutoka kwenye bomba, baharini. Katika
tukio hilo watu wasiofahamika, wakiwa na mabomu na baadhi ya milipuko,
walilitelekeza boti lao na kutoweka kusikojulikana kwa kupiga mbizi
baharini baada ya walinzi wa doria kuwakurupusha kwa kurusha risasi
hewani.
“Tunaomba tupatiwe vitendeakazi kwa ajili ya kikosi chetu
kinachofanya kazi kubwa ya kupambana na uhalifu mbalimbali bandarini
hasa magari ili kukiwezesha kikosi hicho kufanya kazi yake kwa ufanisi,”
alieleza Kakoko. Dk Mpango ameahidi kuipatia TPA vitendea kazi ambavyo
viko ndani ya uwezo wake kama Waziri ili kuongeza udhibiti wa eneo la
maji ya bahari lenye bomba la mafuta.
“Ninawapongeza sana kwa kufanikisha kuwadhibiti maharamia hao ambao
wamekuwa wakitumika kuharibu miundombinu ya bomba la mafuta na kuharibu
mita za kupimia mafuta, nawaahidi kuwatimizia maombi yenu ya vifaa
ambavyo viko ndani ya uwezo wangu,” alisema Dk Mpango.
Alisema vitendo vinavyofanywa na wahalifu hao vinakwamisha juhudi za
serikali za kuimarisha miundombinu yake na kusababisha hasara kwa wenye
mafuta na kuikosesha serikali mapato kutokana na vitendo hivyo vya
kutoboa bomba na kuiba mafuta.
Mbali na kushuhudia boti iliyokamatwa pamoja na vifaa vyake ikiwemo
injini na magaloni ya mafuta, Dk Mpango alipewa maelezo kuhusu mchakato
unaoendelea wa kufunga mita mpya za kupimia mafuta. Kakoko ameeleza kuwa
mchakato unaendelea vizuri na kwamba huenda ukakamilika mapema mwakani,
hatua itakayosaidia kuongeza mapato ya serikali bandarini hapo.
Chanzo Habari Leo
0 comments:
Post a Comment